WAKILI Kuawayawaya Stephen Kuwayawaya, amemshauri Rais Samia Suluhu kuwa makini na watendaji wa ofisi yake. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Kuwayawaya ametoa ushauri huo jana tarehe 29 Aprili 2021, akizungumza na wanahabari jijini Dodoma.
Kuwayawaya amemshauri Rais Samia kuwaondoa watendaji walioko katika ofisi yake, ambao hawatekelezi majukumu yao ipasavyo.
“Ukimuangalia Samia anaendeshaje nchi unakosea, yeye ni msimamizi na muangalizi, kinachotakiwa kwa Samia ni kuwa na jicho kali kuangalia taasisi yake na waliomo, na kugundua watu wengine ambao hawaendi kwa mujibu wa maelekezo au mwenendo wa taasisi yenyewe, yaani hicho tu akiwa smart kila kitu kitakwenda vizuri,” amesema Kuwayawaya.
Wakili huyo amesema, Rais Samia anapaswa kuwa makini na wasaidizi wake, kwa kuwa ikitokea dosari yoyote atakayenyooshewa kidole ni yeye.
“Rais kama rais ni taasisi, kwa hiyo utendaji kazi wa rais sio utendaji wa mtu mmoja. Yeye anakuwa msimamizi na msemaji wa taasisi, lakini kinachofanya kazi hasa ni watu ambao wako kwenye hiyo taasisi ya rais,” amesema Kuwayawaya.
Samia ambaye ni Rais wa Awamu ya Sita wa Tanzania, aliapishwa kushika nafasi hiyo tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha Hayati Dk. John Magufuli, aliyefariki dunia tarehe 17 Machi 2021, kwenye Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam.
Yaani kila wakili akitoa ushauri imekuwa ni story?
Kwanini msitoe maoni ya chama cha mawakili? TLS ni msemaji wa mawakili