IMEELEZWA kuwa kutelekezwa kwa baadhi ya miradi ya ujenzi wa barabara na madaraja katika mkoa wa Songwe imetokana na baadhi ya wakandarasi waliopewa zabuni kutokuwa na mitaji ya kutosha huku wengine wakionesha vifaa visivyo vyao.
Udanganyifu huo umesababisha miradi mingi kukwama kutokana na wakandarasi hao kukodi vifaa huku wengine wakitumia mikokoteni ya kukokotwa na ng’ombe kubebea zana za ujenzi hali inayofifisha uharakishwaji wa miradi ya maendeleo. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe …(endelea).
Hayo yamebainika juzi tarehe 7 Machi 2023 katika kikao cha bodi ya barabara mkoani Songwe kilichoshirikisha wajumbe mbalimbali wakongozwa na mkuu wa mkoa.

Kikao hicho kililenga kujadili ajenda ya hali ya barabara,utekelezaji wake na changamoto zilizopo.
Aidha, Meneja TARURA mkoa wa Songwe, Mhandisi Kilian Haule alisema alikiri kuwepo kwa wakandarasi hao wababaishaji.
”’Mwaka huu wa fedha tumewasilisha bajeti ya Sh bilioni 16 zitakazofanya kazi ya matengenezo ya barabara na madaraja kwa mkoa wa Songwe.
“Ninakiri kuwa wakandarasi wasiokuwa na sifa wampelekea baadhi ya miradi kukwama lakini mwaka huu tutatumia mfumo wa Data Base kuwatambua ili kuwa na uhakika na kazi zao” alisema Mhandisi Kilian.
Akizungumzia hali hiyo Aloyce Mdalavuma mjumbe wa bodi ya barabara,alisema kuna umuhimu Wakala wa Barabara Vijijini – Tarura kufungua njia zilizopo katikati ya mkoa kwani zinaungana na wilaya ya Mbozi kwenda wilaya ya Songwe hadi mikoa ya Rukwa na Katavi ambako ndiko waliko wakulima watakaoweza kusafirisha mazao yao kirahisi.
Mmoja wa wakazi wa mkoa huo. Samwel Mwampashe alisema kuna baadhi ya maeneo hasa vijijini ambako wakulima wanashindwa kusafirisha mazao yao kutokana na ubovu wa barabara huku madaraja mengine yakitelekezwa na wakandarasi kabla ujenzi wake kukamilika.
Naye Anna Kayange mkazi wa Ileje,alisema serikali imetoa fedha nyingi kujenga miradi ya aina hiyo lakini ile ya vijijini bado ni kizungumkuti.
Leave a comment