SERIKLI imesema, imeweka mikakati ya kuhakikisha inawawezesha na kuwajengea uwezo wakandarasi wazalendo, ili waweze kutekeleza miradi mikubwa badala ya kusubiri wakandarasi wa kigeni. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Na kwamba, wakandarasi wa kigeni wanaotekeleza miradi mikubwa nchini, watalazimika kushirikiana na wazawa ili kuwapatia ujuzi.
Kauli hiyo imetolewa na Elius Mwakalinga, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi leo tarehe 8 Januari 2020, wakati akifungua kikao cha mashauriano kati ya Wizara ya Ujenzi na wakandarasi wazalendo, kuhusu ushiriki wao katika miradi ya ujenzi.
Mwakalinga amesema, kutokana na kuwepo kwa upungufu mbalimbali katika sheria ya kuwatambua wakandarasi wa ndani, kwa sasa kuna mazungumzo ili kurekebisha sheria hiyo.
Amesema, wakandarasi wa ndani wanakumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo kutowezeshwa kiuchumi, hivyo kushindwa kufanya kazi zao.
“Tunachotaka kufanya sasa ni kuhakikisha wakandarasi wa kigeni pamoja na wakandarasi washauri, wanapokuja katika kutekeleza miradi yao mikubwa, ni lazima watoe elimu ya matumizi ya mitambo mikubwa wanayoitumia.
“Pia watoe elimu kwa wakandarasi wa ndani katika maeneo ambayo hawajaweza kuyajua, ili kuwawezesha kupata uelewa wa kutosha. Wakandarasi wa wazalendo wakiishajengewa uwezo wa kiuchumi na kielimu, itakuwa rahisi wao kwenda kutekeleza miradi mikubwa,” amesema.
Leave a comment