WAJASIRIAMALI wilaya ya Temeke mkoa wa Dar es Salaam, wameeleza sababu zinazopelekea vikundi vya kuweka akiba na kukopa mikopo kufa na kuacha maumivu kwa wanachama walioweka fedha zao. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza katika mkutano wake na wanachama wa vikundi vya VICOBA Endelevu wilayani humo, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Temeke, Johari Mkonde amesema miongoni mwa sababu za vikundi hivyo kufa ni pamoja na usimamizi mbovu kuhusu masuala ya fedha na ukiukiwaji wa katiba za vyama hivyo.
Johari ambaye pia ni Mratibu wa Taasisi ya VICOBA Endelevu-SDA, amesema kitendo cha baadhi ya wanachama kutolipa mikopo yao kwa wakati na wengine kukimbia na fedha za vikundi, ni miongoni mwa sababu za vikundi hivyo kutotimiza malengo yake na hatimaye kuvunjika.
“Ulipaji wa mikopo umekuwa changamoto kubwa. Wasimamizi wa mikopo wanatakiwa kutowalea wanaogoma kulipa mikopo kwa wakati, inatakiwa wahakikishe waliokopa wanalipa madeni yao kwa wakati ili hizo fedha ziwanufaishe wanachama wengine,” amesema na kuongeza Johari.
“Kikundi kikishirikiana katika kufuatilia ulipaji wa madeni, wanaokopa hawawezi kukimbia na pesa, inatakiwa tuwe na msimamo ili tuweze kufikia malengo ya kujikwamua kiuchumi. Wale wanaohusika na marejesho waendelee na majukumu yao.”
Katika hatua nyingine, Johari amewahimiza wajasiriamali kusajili vikundi vyao vya kuweka akiba na kukopa mikopo serikalini, ili viweze kutambulika na kupata fursa zinapojitokeza
Johari ameeleza kwamba, changamoto ya wajasiriamali kutosajili serikalini vikundi vyao, imepelekea kutotambulika pindi fursa zinapojitokeza, na kuwataka wanachama wa vikundi hivyo kufuata taratibu na masharti ya usajili, ili wasajili vikundi vyao.
Leave a comment