WAHITIMU wa elimu ya dini wa Chuo cha Jamiah Ahmadiyya kilichopo Kihonda Maghorofani katika manispaa ya Morogoro wametakiwa kuwa waadilifu na mfano mzuri kwa jamii pindi wanapoenda kutekeleza majukumu yao ya kufundisha. Anaripoti Ashura Kazinja, Morogoro … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 6 Disemba, 222 na Amiri na Mbashiri Mkuu wa Jumuiya ya Waislam wa Ahmadiyya Tanzania, Sheikh Tahir Mahmoud Chaudry kwenye mahafali ya 38 ya kuwaaga wahitimu wanaomaliza masomo yao chuoni hapo.
Alisema kuwa ili waweze kuheshimiwa na kuthaminiwa katika jamii ni vyema wakawa mfano mzuri kwa kutenda yaliyo mema.
Sheikh Chaudry aliwasisitizia wahitimu hao kujiendeleza zaidi kielimu hasa kwa kusoma vitabu mbalimbali vitakavyowasaidia kupata uelewa na ujuzi katika elimu hiyo ya dini ya Kiislam.
“Jambo la muhimu sana ni vitendo, kama tumemuamini Mtume Muhammad na Quruan basi tufate matendo yake, kwa kuwa sisi ni walimu hivyo ni vyema kufuata matendo yote mema kama ishara ya kumtii Mungu” alisema Sheikh Chaudry.
“Mwenendo wetu ni muhimu sana jinsi tunavyoishi au kukaa na watu, tukitoka nje muonekano wetu na mavazi yetu yakoje, tabia zetu na hata namna ya kuongea tunatizamwa na watu tunaongea nini na kwa namna gani” aliiongeza
Kwa upande wake Mkuu wa chuo hicho Sheikh Mahmoud Bhatti alisema kuanzia mwakani wanatarajia kuboresha zaidi mazingira pamoja na mitaala ya kufundishia ili waweze kutoa elimu bora zaidi.
“Miaka hii miwili tutaitumia kuboresha mitaala na kuangalia vitu gani havipo ili viongezwe kwenye silabasi, mwakani tunapoanza tunaanza mtaala mpya, Mungu atatusaidia kufikisha malengo yetu ya kuboresha elimu” alisema Sheikh Bhatti.
Akitoa ripoti ya chuo kwa mwaka 2022 Mwalimu Shamuni Juma alisema kuwa pamoja na masomo ya darasani pia chuo kimeweka utaratibu wa program maalum ambayo lengo lake ni kuwajenga na kudumisha nidhamu za wanafunzi hao.
Mwalimu Shamuni aliongeza kuwa hadi sasa chuo kimefanikiwa kuwapeleka wanafunzi 20 nchini Ghana ambao wameenda kujifunza zaidi elimu ya dini , wakiwemo wanafunzi wengine watatu walioenda mwaka huu.
Hata hivyo mahafali hayo ya 38 yameenda sambamba na ufunguzi wa maktaba mpya yenye vitabu mbalimbali ikiwemo Quruan na Kompyuta, ambayo ujenzi wake umegharimu shilingi milioni 29.
Leave a comment