SERIKALI imeombwa kuweka utaratibu wa upatikanaji wa fedha za kununua visanduku vya tiba kwa wanyama na kuweza kumkabidhi kila wanafunzi ili wanafunzi wanaomaliza elimu ya juu ya mifugo waweze kuwa navyo kufuatia kushindwa kufanya kazi vizuri wanapomaliza masomo kutokana na kukosekana kwa visanduku hivyo mahali wanapokwenda. Anaripoti Christina Haule … (endelea).
Ombi hilo lilitolewa jana na mwanzilishi wa kitivo cha tiba ya mifugo kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) Prof. Beda Kessy wakati wa sherehe za siku ya tiba ya wanyama duniani iliyofanyika katika viwanja vya hospitali ya wanyama katika ndaki ya tiba ya wanyama na sanyansi za Afya SUA.
Prof. Kessy amesema kuwa mara nyingi wanafunzi hao wamekuwa wakitayarishwa vizuri kielimu wawapo chuoni hapo lakini wanapotoka hapo wakiwa na digrii zao na kuajiriwa kwenye wilaya au maeneo mengine hushindwa kufanya kazi zenye ubora kwa tiba za wanyama kufuatia kukosekana kwa visanduku hivyo.
Hivyo amesema ni vema serikali ingeliona hilo na kutenga bajeti kwa ajili ya manunuzi ya visanduku hivyo kwa manufaa ya wanyama na Taifa kwa ujumla.
Naye Makamu Mkuu wa chuo hicho Prof. Raphael Chibunda amewataka wamiliki wa wanyama kutambua kuwa wao daktari wa mifugo ni muhimu sana kwao na kwa wanyama wao pia.
“Kwa mfugaji iwe ni mbwa, paka, farasi au kuku nafahamu kuwa mnawapenda wanyama wenu lakini kwenu daktari wa mifugo ni muhimu sana kwenu kama alivyo kwa wanyama wake,” amesema.
Amesema kuwa kwa Ndaki ya tiba ya wanyama kujitolea kujitolea kufanya matibabu na ushauri wa bure kwa wamiliki wa wanyama ni nafasi muhimu ya kuzidi kuimarisha mahusiano yao na wanyama na madaktari wao.
Hivyo aliwaomba wamiliki hao kuwa mabalozi wa tiba ya wanyama mahali wanapokaa na kwamba wataalam na vifaa vilivyopo kwa sasa SUA kwa ajili ya Tiba ya mifugo havitumiki kiasi cha kutosha, huku afya za wanyama zikiwa haziko nzuri sana sambamba na magonjwa ya hatari kama kichaa cha mbwa kuendelea kutishia uhai wa binadamu hapa nchini.
Alishauri watanzania wanaoifahamu fursa hiyo kuitua vyema na kuitumia kuwaelimisha watanzania wengi ambao hawajui juu ya uwepo wa taaluma na huduma hizo hapa nchini.
Amesema, ifahamike kwamba uboreshaji wa maisha ya wanyama sit u utawasaidia wanyama na wamiliki wao bali pia itasaidia kuboresha ajira, kuboresha mazao ya wanyama nchini na hivyo kuongeza kipato na uchumi wa nchi.
Leave a comment