WAKALA wa Barabara Tanzania (Tanroads), umekubali kuongeza muda wa notisi kwa wamiliki wa nyumba na vibanda vya biashara, vilivyopo katika hifadhi ya barabara ya Morogoro, kwenye maeneo ya Ubungo-Kimara Stopover, mkoani Dar es Salaam, Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumapili, tarehe 18 Julai 2021 na Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Kherry James, katika mkutano wa wananchi hao, wabunge, Kitila Mkumbo (Ubungo) na Issa Mtemvu (Kibamba), pamoja na madiwani wa kata zilizoguswa na bomoamoboa hiyo.
Kherry amesema kuwa, Tanroads itatoa muda wa nyongeza tarehe 21 Julai mwaka huu, baada ya wakala huo kupewa idhini na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.
Awali, wananchi hao walipewa notisi ya mwezi mmoja kuondoka katika maeneo yao, ambapo walitakiwa kukamilisha zoezi hilo mwezi huu.
“Barua yenu mliyoniletea ilikuwa na hoja sita ikiwemo fidia, malalamiko ya umbali wa hizo mita 90, lakini hoja kubwa ilikuwa ni notisi iliyotolewa ni ya muda mfupi sana, kwamba mnaondokaje. Niliwakutanisha wawakilishi wenu na meneja wa Tanroads Dar es Salaam na wasaidizi wake, wenzenu waliwawakilisha vizuri walieleza hoja na Tanroads wakasema wapo tayari kuongeza muda wa notisi waliotoa, ” amesema Kherry.
Kherry ameongeza “changamoto tuliyonayo ni waongeze muda gani? Mweye mamlaka ya kuongeza muda ni meneja wa Tanroads, lakini mwenye mamlaka ya kujua ni muda gani uongezwe ni Wizara ya Ujenzi.”
Kuhusu ombi la fidia, Kherry amesema Serikali italifanyia kazi suala hilo.
“Hii ndio hatua ya awali kuhusu kipengele cha muda wa notisi, kuhusu hoja zingine zilizonaki kwa sababu muda utaongezwa, ile kamati yenu nitaipa fursa kukaa pamoja mezani, ili tujadiliane hizo hoja sita na kuzipatia majibu.Hoja zote zitapata majibu,” amesema Kherry.
Kherry amesisitiza kuwa, hakuna mgambo wala Polisi atakayewasumbua wananchi hao ikiwemo kuwaondoa, hadi muafaka wa suala lao upatikane na ataitisha mkutano mwingine baada ya kupata majibu ya kutoka Wizarani.
Leave a comment