HOSPITALI ya Rufaa ya Bugando (BMC), inatarajia kujenga jengo maalum litakalowahudumia wagonjwa 800 kwa siku ambao wanatibiwa kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), anaandika Moses Mseti.
Hatua hiyo itasaidia kuondoa malalamiko ya muda mrefu yaliyoikuwapo hapo ambayo yalikuwa yanahusiana na msongamano wa wagonjwa.
Kauli hiyo imetolewa leo na Dk. Abel Makubi, Mkurugenzi Mkuu wa BMC, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uzinduzi wa jengo hilo linalotarajiwa kuzinduliwa Agousti 25 mwaka huu na Waziri wa afya, Jinsia, Wazee na watoto, Ummy Mwalimu.
Dk. Makubi amesema siku ya uzinduzi huo wananchi watakaofika hospitalini hapo watapimwa baadhi ya magonjwa bure.
Magonjwa yatakayopimwa bure ni pamoja na shinikizo la damu, magonjwa ya sukari, ukimwi, figo, saratani ya kizazi na matiti ili kutoa fursa kwa wakazi wa mikoa ya kanda ya ziwa kufahamu afya zao.
“Lengo ni kuboresha huduma katika hospitali yetu, pia kuhakikisha wagonjwa wanaopata huduma kupitia NHIF wanapata huduma kwa wakati,” amesema Dk. Makubi.
Kelebe Luteli, Mkuu wa Kitengo cha Bima, amesema katika jengo hilo litakuwa na sehemu maalumu kwa viongozi wa kitaifa na kimkoa na kwamba madaktari bingwa wa watoto na wakina mama na wa upasuaji watapatikana muda wowote.
Leave a comment