CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania kitateua wagombea ubunge, uwakilishi na viti maalum tarehe 22 Agosti 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
CCM ambacho ni chama tawala, kitafanya uteuzi huo ikiwa ni siku tatu kubaki kabla ya dirisha kufungwa la uchukuaji na urejeshaji wa fomu za kuwania ubunge tarehe 25 Agosti 2020.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imeanza kuzitoa fomu za kugombea ubunge tarehe 5 Agosti 2020 ambapo tayari baadhi ya vyama vimeanza kuchukua fomu hizo hususani wagombea wa Chama Kikuu cha Upinzani nchini humo cha Chadema.
Tayari kura za maoni zimefanyika zikihusisha wagombea zaidi ya 8,000 katika majimbo 264 ya Tanzania Bara na Zanzibar na vikao vya jimbo, wilaya na mikoa ya kuwajadili watiania hao vimekwisha kufanyika.
Tarehe 17 na 18 Agosti 2020, kitafanyika kikao cha sekretarieti ya halamshauri kuu ya CCM Taifa na tarehe 19 Agosti 2020 itakuwa ni kikao cha kamati ya usalama na maadili ya chama hicho.
Tarehe 20 na 21 Agosti 2020, kitafanyika kikao cha kamati kuu ambacho kitatoa mapendekezo yake kwa halmashauri kuu juu ya wanachama wake wanaoomba kuteuliwa kugombea ubunge wa majimbo, Viti maalum na uwakilishi.
Tarehe 22 Agosti 2020, kitakuwa kikao cha halmashauri kuu ya CCM ambacho kitafanya uteuzi wa mwisho wa wagombea ubunge, ujumbe wa baraza la wawakilishi na viti maalum.
Kitendo cha CCM kuteua wagombea dakika za mwisho, kitawafanya watakaoshindwa kukosa fursa ya kujiunga na vyama vya upinzani, kwani michakato ndani vyama hivyo itakuwa umehitimishwa.
Soma zaidi hapa
Wagombea ubunge CCM, presha inapanda, presha inashuka
Itakumbukwa katika uchaguzi mkuu mwaka 2015, baadhi ya makada wa CCM waliokatwa kuwania ubunge walihamia upinzani ambako walipitishwa kugombea nafasi hiyo na wakaibuka washindi.
Leave a comment