MCHAKATO wa kumpata Naibu Meya wa Manispaa ya Dodoma ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), umeanza huku wagombea waliojitokeza katika kinyang’anyiro hicho wakionywa kutokujihusisha na vitendo vya rushwa, anaandika Mwandishi Wetu.
Akizungumzia mchakato huo, Katibu wa CCM wilaya ya Dodoma, Pili Mbanga, amesema mchakato huo umeanza baada ya Mkurugenzi wa Manispaa hiyo kuwaandikia barua ya kuwasilisha jina la mgombea.
“Mchakato huu ndani ya chama utamalizika ndani ya wiki hii kwa kuwa maelekezo ya Mkurugenzi jina linatakiwa kuwasilishwa Agosti 9, mwaka huu,” amesema Katibu huyo.
Alibainisha hadi sasa wamejitokeza madiwani sita katika kinyang’anyiro hicho akiwemo Naibu Meya wa sasa, Jumanne Ngede anayetetea nafasi hiyo.
Aliwataja wengine ni Msinta Mayaoyao, Ally Mohamed, Abel Shauri, Jakobu Lemanya na Neema Mwaluko.
Aliwataka kutotumia rushwa katika uchaguzi huo kwa kuwa kiongozi mzuri anapatikana bila rushwa.
“Hawatakiwi kutoa au kupokea rushwa na ikibainika ameshinda kwa kutumia rushwa CCM itamuengua,” amesema Mbanga
Kadhalika, Mbanga amesema mchakato wa chaguzi mbalimbali ndani ya chama na jumuiya zake unaendelea na unatarajiwa kukamilika Agosti 5, mwaka huu.
Leave a comment