VIONGOZI wa magereza nchini Nigeria, wameeleza jumla ya wafungwa 1,800 wametoroka jela baada ya watu wenye silaha kuvamia gereza la Owerri, kusini mwa nchi hiyo na kushambulia. Inaripoti mitandao ya kimataifa…(endelea).
Taarifa zinaeleza, watu kadhaa wakiwa na silaha, walivamia gereza hilo usiku na kubomoa ukuta kisha kuruhusu mafungwa hao kutoroka.
Tukio hilo limelaaniwa na Rais wa nchi hiyo, Muhammad Buhari ambapo ameliita kwamba ni tukio la kigaidi. Kwa wiki mbili sasa Rais Buhari yupo London, Uingereza kwa matibabu.
Katika tukio hilo, taarifa zinaeleza wafungwa 35 walikataa kutoroka na sita wamejeruhiwa katika harakati za kutoroka.
Inaelezawa, kundi linalotaka kujitenga na kuwa na uhuru wao – Biafra – ambalo linapigwa marufuku kali na uongozi wa Rais Buhari, linatajwa kuendesha shambulizi hilo.
Uongozi wa gereza hilo lililopo kwenye Jimbo la Imo umeeleza, idadi kamili ya wafungwa waliotoroka ni 1,844.
Wavamizi hao, jana Jumatatu wakiwa na gari aina ya Pick Up na basi, walivamia gereza hilo lililopo katika Mji wa Owerri na kuanza mashambulizi sambamba na kuvunja ukuta.
Maofisa wa gereza hilo wameeleza, silaha zingine zilizotumika kwenye uvamizi huo ni Pamoja na roketi, maguruneti na silaha nyingine katika uvamizi huo.
Rais Buhari ameagiza kukamata kwa washambuliaji hao pamoja na wafungwa waliotoroka.
Leave a comment