JESHI la polisi mkoa wa Dodoma linawashikilia watu wawili kwa makosa ya kutumia vibaya mitandao ya kijamii kwa madai ya kuchochea maandamano ya nchi nzima ambayo yanakusudiwa kufanyika Aprili 26 mwaka huu. Anaripoti Dany Tibason … (endelea).
Maandamano hayo yaliyopangwa kufanyika Aprili 26 mwaka huu, yanayohamasishwa na Mange Kimambi anayeishi nchini Marekani kwa lengo la kupinga mwenendo wa nchi kwa sasa.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema jeshi hilo limewakamata watu wawili ambao wanatumia vibaya mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuchochea maandamano nchi nzima kinyume na taratibu za nchi.
“Kwa muda mrefu sasa kwa makusudi na wakitambua kuwa ni kosa kisheria, baadhi ya watu wasiopenda amani na utulivu wa nchi wanatumia vibaya mitandao ya mawasiliano kuvunja sheria na kuhamasisha chuki dhidi ya serikali kuhamasisha maandamano yasiyo halali yenye viashiria vya kuvuruga amani ya nchi waliyopanga kuyafanya nchi nzima siku ya tarehe 26/4/2018.
“Hapa Dodoma tumekamatwa watu wawili ambao kwa makusudi kwa kutumia mitandao ya simu wanasambaza maneno yenye uchochezi dhidi ya serikali, wanatishia usalama wa nchi wanahamasisha maandamano ya nchi nzima yenye viashiria vya uvunjifu wa amani,” amesema Muroto.
Kamanda Muroto amewataja waliokamatwa kuwa ni Amandus Machali (31) dereva wa NHIF na mkazi wa Kigamboni geti jeusi jijini Dar es Salaam na Yuda Mbata (29), mkulima na mkazi wa kijiji cha Mpanatwa wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.
Katika tukio lingine Kamanda Muroto amesema kumetokea vifo vya watu watatu wa familia moja katika kijiji cha Gwandi katika wilaya ya Chemba mkoani Dodoma kutokana na watu hao kuangukiwa na ukuta wa nyumba wakiwa wamelala.
Amesema kuwa tukio hilo lilitokea Machi 18, mwaka huu usiku katika kijiji hicho na kusema chanzo cha vifo hivyo ni kutokana na kuta za nyumba kulowana na maji ya mvua zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali mkoa wa Dodoma.
Aliwataja waliokufa kuwa ni Misa James (25) Happy James (2) na Mbalu James ambaye hakumtaja umri wake.
Leave a comment