WAKATI mchakato wa Uchaguzi Mkuu nchini Kenya ukizidi kupamba moto, imebainika kuwa wafu 250,000 wameandikishwa katika orodha ya wapiga kura katika vitabu vya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini humo (IEBC). Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hayo yameelezwa jana tarehe 1 Aprili jijini Nana Kamishna wa IEBC, Justus Nyang’aya, ambaye amefafanua kuwa itakuwa vigumu kuondoa majina yote ya wafu katika orodha hiyo ya wapigakura.
“Tumepokea karibu majina 250,000 kutoka kwa idara inayosajili vifo. Ukweli ni kuwa tutajitahidi sana kuyaondoa majina yao kwenye orodha ya waliosajiliwa lakini si wote kwa sababu watu hufa kila siku hata siku ya uchaguzi wenyewe bado kutakuwa na vifo.
“Hoja muhimu ni kuwa wale ambao wamefariki na majina yao yako kwenye usajili wa wapigakura hawatashiriki uchaguzi huo. Hakuna mfu atakayefufuka kisha kupiga kura,” amesema Nyang’aya.
Katika chaguzi za awali inaelezwa, idadi ya waliojitokeza kupiga kura katika baadhi ya maeneo huzidi asilimia moja au idadi ya wapigakura waliosajiliwa katika kituo fulani.
Hilo limeibua madai ya kuendelezwa kwa udanganyifu huku hata watu waliofariki wakihesabiwa kama waliopiga kura na kuzua maswali iwapo shughuli hiyo inafanywa kwa uwazi.
Tarehe 1 Machi, Afisa Mkuu Mtendaji wa IEBC, Hussein Marjan alisema tume hiyo imechelewa kuyaondoa majina ya wafu kwenye orodha ya usajili wa wapigakura kwa sababu haikuwa imeajiri kampuni ya kufanya ukaguzi na kuyaondoa.
Alisema wananchi watapewa nafasi ya kuthibitisha iwapo wamesajiliwa kuwa wapigakura kati ya Aprili na Mei.
Aidha, alisema tayari IEBC imekamilisha mchakato wa utoaji wa tenda kwa kampuni ya KPMG ambayo itakagua majina ya wapigakura kisha kutoa mapendekezo ambayo tume itayatekeleza kabla sajili kupigwa msasa kwa mara ya mwisho.
Katika uchaguzi mkuu huo Kenya inatarajiwa kuwa na wapiga kura milioni 25 hata hivyo katika maboresho ya daftrai la wapiga kura awamu ya kwanza mwaka jana ilisajili wapiga kura milioni 1.5 badala ya milioni sita wakati awamu ya pili mwaka huu imesajili wapiga kura milioni 2.5 badala ya milioni 4.5.
Aidha, katika uchaguzi huo mahasimu wawili Naibu Rais Wiliam Ruto anatarajiwa kuvaana na kiongozi wa upinzani nchini humo, Raila Odinga anayeungwa mkono na Rais Uhuru Kenyatta.
Leave a comment