WAFANYAKAZI nchini wametakiwa kuendelea kuhamasika kujitokeza kwa wingi wakati wa maandamano kwenye siku ya maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi ili kuweka bayana changamoto zinazowakabili sehemu zao za kazi na kuweze kupatiwa ufumbuzi. Anaripoti Christina Haule … (endelea).
Wito huo ulitolewa jana na Katibu wa Chama Cha Wafanyakazi (TPAWU), Nicholaus Ngowi wakati akizungumzia sherehe za Mei Mosi zinazotarajiwa kufanyika kimkoa katika viwanja vya Jamhuri mkoani Morogoro.
Ngowi amesema kuwa wafanyakazi wanapaswa kutambua kuwa Maadhimisho hayo ni sehemu ya kutoa changamoto zao ikiwemo masuala ya mahusiano yaliyopo sehemu zao za kazi. Aidha aliwataka waajiri kuendelea kutoa haki kwa wafanyakazi hasa pale wanapotimiza wajibu wao.
Naye Mratibu wa sherehe za Mei Mosi Mkoani hapa Mgassa Chimola amewaomba waajiri wilayani na mkoa mzima wa Morogoro kuwaruhusu watumishi kuhudhuria maadhimisho hayo huku wakileta bidhaa mbalimbali kwa ajili ya maonesho na elimu kwa jamii.
Chimola ambaye pia ni Katibu wa Chama Cha wafanyakazi (TUICO) mkoa, amesema kuwa maadhimisho hayo kimkoa yatafanyika katika uwanja wa Jamhuri Manispaa ya Morogoro ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa ni mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dk. Kebwe Steven Kebwe.
Amesema, maadhimisho hayo yataanza na maandamano yatakayoanzia ofisi za TUICO mkoa zilizoko barabara ya stesheni Manispaa ya Morogoro ambapo kauli katika maadhimisho hayo ni “kuunganishwa kwa mifuko ya hifadhi za jamii kulenge kuimarisha maslahi ya wafanyakazi”.
Naye Mwenyekiti wa maandalizi ya sherehe hizo kimkoa, Mohamedi Simbeye amewaasa wafanyakazi kujiunga kwenye vyama vya wafanyakazi ili waweze kuwa na umoja wa kuwatetea hasa kwenye masuala yanayohusu maslahi yao.
Aidha Simbeye ambaye pia ni Mwenyekiti wa TUCTA mkoa wa Morogoro amesema kuwa maandalizi ya mwaka huu yamejitahidi kuondoa dosari ndogondogo zilizokuwa zikijitokeza kwenye maadhimisho ya nyuma ikiwemo waajiri kutofikisha zawadi kwa mshindi kama ilivyokusudiwa.
“Kwa sasa changamoto zimetatuliwa, tunapokea zawadi mapema za washindi wote kabla hatujaingia uwanjani, na mshindi anakabishiwa zawadi yake papo hapo kuanzia kwa viongozi wa wilaya hadi mkoani,” amesema.
Leave a comment