CHAMA cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) kimekerwa na baadhi ya wanasiasa kuwawajibisha na kuwadhalilisha watumishi wa Umma. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akisoma risala ya TALGWU, Mkuu wa Idara ya Habari na Uhusiano Kimataifa wa TALGWU, Shani Kibwasali kwa niaba ya Katibu Mkuu TALGWU, alisema kuwa kwa sasa imeibuka tabia ya wanasiasa kuwadhalilisha watumishi wa serikali ya Umma.
Shani alisema kitendo cha baadhi ya wanasiasa kutumia madaraka yao vibaya kwa kuwadhalilisha na kuwaweka kana mahabusu wanachama bila sababu za msingi na kutozingatia sheria zinazowapa Mamlaka hayo ni kushusha heshima ya hadhi heshima na morali ya watumishi.
“Hivyo tunaomba serikali kukemea vitendo hivi kuwaelekeza viongozi wanasiasa kuzingatia, sheria, kanuni na taratibu za masuala ya nidhamu kwa watumishi.
“Endapo italazimu mtumishi kuwekwa mahabusu kwa hofu ya uvunjifu wa amani basi matakwa ya kisheria yazingatiwe,” alisema Shani.
Alisema kero nyingine ni kukosekana kwa miundombinu na huduma za msingi katika maeneo mapya yalipohamishiwa ofisi za halmashauri ili kusogeza huduma kwa wananchi.
Alisema kuwa watumishi wamehamishwa katika maeneo yao bila kuzingatia maandalizi ya kutosha, huku maeneo mengi hakuna majengo yenye hadhi ya ofisi, huduma ya maji,huduma ya kijamii, usafiri, umeme, nyumba za kuishi pamoja na huduma nyingine za msingi.
Shani akiendelea kutaja changamoto alisema pamoja na serikali kuwarejesha kazini wanachama waliodolewa kwa kukosa cheti cha ufaulu wa elimu ya kidato cha nne ambao waliajiliwa kabla ya Mei 20 mwaka 2004 na kuhaidi kulipa malumbikizo ya mishahara kwa miezi yote lakini yapata miezi 20 sasa hawajalipwa.
Jambo lingine alisema ni wastaafu kutolipwa mafao yao kwa wakati jambo balo si jema kwa watumishi hao.
Kwa upande wa Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga akijibu lisala ya Talgwu, alisema kuwa ni kosa kwa wanasiasa kuvuka mipaka kwa kuwawajibisha watumishi.
Alisema mwanasiasa anatakiwa kutambua mipaka yake ya kufanya kazi bila kuwadhalilisha watumishi na mtumishi anatakiwa kuwajibishwa kwa mujibu wa kanuni na sheria za utumishi.
Leave a comment