WAFANYABIASHARA katika maeneo ya wazi jijini Dodoma, wameulalamikia uongozi wa jiji hilo kwa kuwafurusha katika maeneo hayo ndani ya siku 30. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Wanasema, wamekuwa wakimiliki maeneo hayo zaidi ya miaka 30 na wana miundombinu yote kama vile maji na umeme, pia kufuata taratibu zote za kibiashara ikiwemo leseni.
Wafanyabishara hao wamesema, imekuwa kawaida ya Halmashauri ya Jiji hilo kufanya makusanyo kwao na baada ya muda mfupi, wanawalazimisha kuachia maeneo ya biashara huku wakishindwa kuayendeleza.
Endrew Juma, maarufu kwa jina la Makuku ambaye ni meneja wa Blue Bar jijini humo amesema, yeye ni kati ya waliopewa barua ya kuondoka katika eneo ambapo tarehe 17 Aprili 2019 alilipa Sh. 600,000 fedha ya ushuru wa eneo.
Amesema, kitendo hicho kinasababisha wafanyabiashara kudhoofika na kukwama kimtaji ikiwa ni pamoja na kusababisha wakazi wa Dodoma kukosa huduma.
“Ipo mifano mingi katika Jiji la Dodoma ambapo maeneo waliyokuwa wakiyatumia wafanyabiashara kujipatia kipato kwa kufuata taratibu zote, wamefukuzwa na hakuna kinachoendelea.
“Lipo eneo la Stendi ya Jamatini ambapo kwa sasa hakuna kinachoendelea na sasa pamekuwa kichaka, Stendi ya Mkoa na maeneo ya jirani walifukuzwa na hakuna kinachoendelea,” amesema.
Na kwamba hata kilipojengwa choo cha kisasa, hakuna kinachoendelea “mkurugenzi wa jiji, Godwini Kunambi alilazimika kujenga ukuta mkubwa na choo cha kisasa kwa fedha za wafadhili, lakini mpaka sasa choo hicho na ukuta havitumiki.”
Mkurugenzi Kunambi alipotafutwa kufafanua, amesema Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA), wakati huo ilikosea kuingia nao mikataba.
Hata hivyo, amesema wapo waliopewa barua za kuondoka kulingana na uboreshaji wa eneo husika ikiwa ni kuanzia miezi sita hadi miaka mitatu.
Patrobas Katambi, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma amesema, uongozi wa jiji unatakiwa kueleza kuwa, wanapotaka kuwaondoa wafanyabiashara hao, wanataka kuweka nini.
Leave a comment