MEYA wa Manispaa ya Kinondoni, Songoro Mnyonge amesema zaidi ya wafanyabiashara 45,000 waliokuwa kwenye mfumo rasmi mkoani Dar es Salaam wamegeukia umachinga katika kipindi cha miaka mitano iliyopita. Anaripoti Noela Shilla, TUDARCo … (endelea).
Songoro ambaye Diwani wa Kata ya Mwananyamala (CCM) ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam leo tarehe 17 Septemba, 2021 wakati akizungumza katika uzinduzi wa kitabu cha mpango wa kuwapanga upya na vizuri wafanyabiashara wadogo maarufu katika wamachinga.
Ameongeza kuwa kwa upande wa Manispaa ya Kinondoni kila mwezi wafanyabiashara 150 hufunga biashara zao sawa na wafanyabiashara 9,000 kwa miaka mitano iliyopita.
“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa hiki ni kilio cha muda mrefu kwa manispaa ya Kinondoni na wengina nakuahidi tutashirikiana na wakuu wa wilaya, makatibu tawala na maofisa watendaji wa kata kuhakikisha yote ulioagiza tunatekeleza kwa asilimia 100 kwa sababu unakwenda kurudisha nidhamu,” amesema.
Amesema kwa miaka mitano au sita iliyopita kumekuwa na wimbi la wafanyabiashara wengi ambao wanafunga biashara rasmi na kuhamia umachinga.
“Kinondoni huwa tunapokea taarifa ya biashara zinazofungwa ambapo kila mwezi ni biashara 150 zinafungwa na hii ni kwa zaidi ya miaka mitano iliyopita.
“Kwa hesabu za Kinondoni, zaidi ya wafanyabiashara rasmi 9,000 wamekuja kutoa tamko la kufunga biashara ili wasitambulike kwenye mfumo.
“Wanapofunga biashara wanapeleka tamko Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Lakini tumebaini wafanyabiasharta hawa wanakwenda kuwa wamachinga.
“Nimeuliza mameya wenzangu hali ni hiyohiyo. Tulikuwa tunachukua takwimu za mkoa mzima na kubaini mpaka sasa ni zaidi ya wafanyabiashara 45,000 waliokuwa kwenye mfumo rasmi wamebadilika na kuwa wamachinga,” amesema.
Aidha, aliwaonya viongozi wenzake ambao wanadaiwa kuingia kwenye biashara ya kuleta wamachinga kutoka mikoani na kuwaleta jijini Dar es Salaam.
Leave a comment