VIONGOZI kadhaa ulimwenguni, wamechanjwa kwa ajili ya kujikinga na virusi hatari vya corona (Covid 19). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Miongoni mwa wanaotajwa kuwa tayari wamepokea chanjo hiyo, ni pamoja na Rais wa Ghana, Nana Akufo-Addo; rais wa sasa wa Marekani, Joe Biden; Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu; Rais wa Ushelisheli, Wavel Ramkalawan na Mwanamfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin Salman.
Rais Akufo Addo, alipokea dozi yake ya kwanza ya chanjo ya Covid-19 Jumatatu, iliyopita kama ishara ya kuwathibitishia raia wake, kwamba chanjo hiyo ni salama.
Rais huyo wa Ghana na wenzake, wameamua kupata chanjo hiyo hadharani, ili kuonesha uongozi na jukumu la uwajibikaji katika kueneza imani katika chanjo.
Pamoja na Shirika la Afya ulimwenguni (WHO), kusisitiza kuwa njia fupi zimetumiwa katika kutengenezwa na kuidhinishwa kwa chanjo, bado haijatosha kuwashawishi baadhi ya watu wanaodai kuwa chanjo hizo zimeharakishwa na hivyo, si salama.
Naye Biden, hata kaba ya kuingia Ikulu ya Marekani, alipokea chanjo na alionyeshwa moja kwa moja na kituo cha televisheni akipokea chanjo ya Corona.
Alikuwa anaonyesha kuwa alikuwa pale na “hakuna la kuhofia. Alifanya tendo hilo, tarehe 21 Disemba mwaka jana.
Waziri Mkuu Netanyahu, Rais Wavel Ramkalawan na Mwanamfalme Mohammed, nao walipokea chanjo zao ili kuthibitishia raia wao kuwa chanjo hiyo, iko salama.
Rais Wavel Ramkalawan aliandika historia ya kuwa kiongozi wa kwanza wa Afrika kupokea chanjo ya corona. Aliandika historia hiyo, tarehe 10 Januari mwaka 2021.
Rais wa Uselisheli alichukua chanjo iliyotengenezwa nchini Uchina-Sinopharm na hivyo, kuanzisha mwanzo wa mpango wa nchi hiyo wa chanjo.
Tarehe 17 Februari mwaka huu, Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, alipokea chanjo yake katika hospitali ya Khayelitsha – hospitali ya umma – akionyeshwa moja kwa moja kwenye televisheni.
Hospitali ya Khayelitsha, ipo katika moja ya miji masikini zaidi nchini humo.
Kwa njia ile, rais Ramaphosa, alitumia jiwe moja kuwauwa ndege wawili: Kuonyesha kwamba chanjo ya virusi vya corona ya Johnson & Johnson ni salama na kwamba ni sawa kwenda katika hospitali ya umma kupokea chanjo ya corona.
Baadae akatuma ujumbe wa Twitter na kusema “ulikua wa haraka, rahisi na usioumiza.”
Tarehe 18 Februari, Makamu wa rais Constantino Chiwenga alipokea chanjo ya kwanza ya corona nchini mwake, akionyeshwa moja kwa moja kwenye televisheni.
Magharibi mwa Afrika, Rais Macky Sall alipokea chanjo ya Sinopharm, iliyotengenezwa na Uchina katika kasri la rais tarehe 25 Februari.
Mfalme Mohammed wa VI alizindua mpango wa chanjo Februari 28 akiwa mtu wa kwanza nchini humo kupatiwa chanjo ya Covid-19 katika kasri la ufalme. Morocco, ni moja ya mataifa yenye mpango mkubwa zaidi wa kitaifa wa chanjo.
Wizara ya afya ilikuwa imeeleza bayana kuwa wahudumu wa afya, usalama, na waalimu pamoja na watu wenye umri wa kuanzia miaka 75, watafuatia kupokea chanjo hiyo.
Nchini Nigeria, ilitarajiwa kwa kiasi kikubwa kwamba Rais Mahammadu Buhari, pia atakuwa mtu wa kwanza kupata dozi ya chanjo ya Covid-19 ambayo itawasili nchini humo Jumanne tarehe 2 Machi mwaka huu.
Dk. Faisal Shuaib, ambaye ni mkuruhgenzi mkuu wa shirika la maendeleo ya huduma za kimsingi za afya (NPHCDA) alisema, rais ana mpango wa kupata chanjo yake huku akionekana moja kwa moja kwenye televisheni kama njia ya kuwatia moyo Wanaigeria kupata chanjo hiyo.
Chanjo hiyo inapatikana chini ya mpango wa COVAX, ambao pia umesambaza chanjo kwa matiafa ya Ivory Coast na Ghana.
Leave a comment