Na Christina Raphael
RAIA 12 wa Ethiopia wanashikiliwa na Polisi mkoani Morogoro kwa kosa la kupita nchini bila kibali au hati ya kusafiria yenye visa ya kuwaruhusu kupita Tanzania.
Watu hao wamekamatiwa eneo la Mikumi wilayani Kilosa wakiwa njiani kuelekea Afrika Kusini kupitia mpaka wa Tunduma.
Kwa mujibu wa Leonard Paulo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, watuhumiwa hao ni Daudi Havarc (30), Belei Kitacho (20), Emasige Tasama (21), Shadio Jamali (18), Daniel Abro (22), Wondim Alficha (22), Ashenaac Malesa (23), Ndita Pundas (18), Azra Lathim (18), Dawiti Petrosi (20), Noerej Daniel (19) na Mhari Samli (30).
Walikamatwa Februari Mosi saa 8:30 usiku katika Barabara ya Iringa, wakiwa kwenye gari aina ya Toyota Noah lenye namba za usajili T786 BHZ lililokuwa linaendeshwa na Hakimu Mustafa mkazi wa Tanga.
Mustafa amesema kuwa akiwa Segera, mkoani Tanga, alipigiwa simu na mmilki wa gari hilo akimtaka afuate abiria Chalinze kisha awapeleke Tunduma. Hakufahamu ni watu wa aina gani.
Kutokana na hali hiyo, Kamanda Paulo ameonya wananchi waache kujihusisha na biashara ya kusafirisha watu wasiowajua. Amesema jeshi la polisi linaendelea kukabiliana na wahamiaji haramu.
More Stories
Takukuru yavimbia wakandarasi, ‘yarejesha’ mil 420 Tanesco
IGP Sirro: Hatufungui kesi za madai, migogoro ya ardhi
Panyabuku waanza kubaini TB