WAJUMBE 40 wa vituo vya taarifa na maarifa nchini wametunukiwa vyeti vya heshima vya elimu ya ajira kwa wanawake na vijana kwa kuanzisha viwanda ikiwa ni pamoja na kubuni miradi ya maendeleo ili kujikwamua kiuchumi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, Kibena Kingo alisema hayo jana wakati akifunga mafunzo ya siku saba ya kuwajengea uwezo wa uzalishaji kiuchumi wajumbe wa vituo vya taarifa na maarifa vilivyo chini ya Mtando wa Jinsia Tanzania (TGNP-Mtandao) waliyoandaa kwa kushirikiana na SUGECO.
Kingo alisema elimu waliyoipata wakiwa wanawake na vijana itawasiaidia kupambana na changamoto ya ukatili wa kijinsia inapotea na kuhakikisha inakwisha katika vijiji na kata kupitia miradi hiyo ya kuwawezesha kiuchumi.
Alisema ikiwa watajituma vuzuri kwenye uchumi wa viwanda kwa kuimarisha kilimo, huku wakihifadhi chakula badala ya kufanya biashara kwa mazao yote wataona kuna tija na kuwaondoa katika kilimo cha kimasikini litakachofanya kushindwa kukabiliana na ukatili wa kijinsia utakapogusa familia zao.
Awali Mkurugenzi wa TGNP Mtandao, Lilian Liundi, alisema wameamua kuwapa vyeti vya heshima mapema wajumbe hao baada ya wenyewe kuonesha nia na hali ya kujituma kijasiliamali na kilimo ili kufikia uchumi wa viwanda.
Alisema mpango wao wa maendeleo wa miaka mitano unazungumzia kilimo na viwanda ambapo alisema kuwa ni matamanio yake kuwaona wanabadilika na kuendana na mpango huo zaidi.
Liundi alisema wanapozungumzia maswala ya uwezeshwaji wa wanawake na wanajamii wanazungumzia haki za kijamii na kwamba wadau au Taasisi inaweza kuwawezesha kiuchumi lakini haki isipoeleweka kwa jamii na wasipoiishi ni vigumu kwao kuona haki ya mwingine.
Naye Meneja uendeshaji na ubunifu kutoka SUGECO, Joseph Massimba, alisema ajenda kuu katika mafunzo hayo ya siku saba ni kuwajengea uwezo wajumbe hao ili waweze kuibua,kuandaa, kuanzisha na kuendesha kwa ufanisi miradi ya kiuchumi itakayochangia kuleta kipato ikiwa ni pamoja na kurudisha maarifa wanayopata kwa jamii wanayotoka ili kuiwezesha jamii wanayotoka kuwa na mtazamo chanya.
Leave a comment