WATU wanaomiliki ardhi mijini, mashambani na vijijini, wametakiwa kulipa kodi ya ardhi kabla ya Januari 2021, vinginevyo watafikishwa kortini. Anaripoti Regina mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Willium Lukuvi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ametoa wito huo wakati akizungumza na Shirika la Utangazaji la Tanzania (TBC), kwenye kipindi cha Ardhio.
Amesema, watu hao wanatakiwa kulipa kwa hiyari na kwamba, wakishindwa kufanya hivyo, watafikishwa mahakamani na kulazimika kulipa na faini.
“Ujumbe wangu wa mwisho kwa mwaka huu, ni kwa wamiliki wote wenye hati za ardhi mijini na mashambani, wanatakiwa kulipa kodi ya ardhi kwa hiyari, mwakani watalazimika kulipa kodi na faini,” amesema.
Kwenye kipindi hicho, Lukuvi amehimiza wanafamilia kumiliki ardhi kwa pamoja kwa mujibu wa sheria ya 1999, ili kupunguza migogoro pale wanapotengana ama mmoja kutangulia mbele ya haki.
Amesema, amekutana na migogoro mingi kuhusu watu kudhulumiana ama kutengana ama mmoja kufariki, ambapo amesisitiza matumizi ya sheria hiyo ni mwarobaini wa migogoro ya ardhi katika umiliki wake.
Leave a comment