RAIA watatu wa China wamefikishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Jiji Dar es Salaam kwa tuhuma za kusafirisha meno ya tembo 1,023 yenye thamani ya zaidi ya Sh 7 bilioni, anaandika Faki Sosi.
Chen Jianlin, Liang hu na Xiao Shaudan ndiyo waliopandishwa kizimbani mbele ya mbele ya Respecious Mwijage Hakimu Mkazi Mkuu.
Elizabeth Mkunde, wakili wa serikali amedai kuwa watuhumiwa hao kati ya mwezi Januari na Novemba mwaka 2013, waliongoza uhalifu wa kusafirsha meno ya tembo 1,023 yenye thamani ya zaidi ya Sh. 7 bilioni kutoka Tanzania Bara kwenda visiwani Zanzibar.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo watuhumiwa walilalamika mbele ya Hakimu Mwijage kuwa wanaonewa kwani kesi hiyo ilishahukumiwa katika Mahakama kuu Kanda ya Mbeya.
Mmoja wa washtakiwa hao Chen Jianlin, aliendelea kulalamika kuwa waliwekwa mahabusu katika Kituo Cha Kati cha Polisi kwa muda wa siku 70 bila kupelekwa mahakamani jambo ambalo ni kinyume cha sheria za Tanzania.
Hakimu Mwijage aliuambia upande wa Mashtaka uwe makini na haki za binadamu kutokana na kuwashikilia raia hao wa China kwa muda mrefu bila kuwafikisha mahakamani.
Upepelzi wa kesi hiyo haujakamilika na washtakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kusikiliza kesi hiyo mpaka itakapopata kibali kutoka Mahakama Kuu.
Kesi hiyo imehairishwa hadi tarehe 31 Januari 2017.
Leave a comment