BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limewatengea wabunge wanawake wenye watoto eneo maalum la kunyonyeshea watoto wao ikiwa ni mkakati wa kuhakikisha watoto hawapotezi fursa ya kunyonya maziwa ya mama licha ya majukumu ya wazazi, anaandika Dany Tibason.
Dk. Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge amelitangazia Bunge kuwa chumba maalum ambacho kitatumiwa na wabunge wenye watoto wachanga kunyonyesha watoto wao kimetengwa na kitakuwa jirani na ukumbi wa Msekwa uliopo ndani ya viwanja vya Bunge, Mjini Dodoma.
“Napenda kutoa tangazo kwa akina mama wabunge ambao wana watoto wadogo, kwa sasa kimetengwa chumba maalum kule kwa Msekwa karibu na chumba cha usalama.
“Hivyo wabunge ambao mna watoto wachanga wakati mkiendelea na shughuli za Bunge mnaweza kunyonyesha watoto na kama mnavyojua Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imetueleza kuwa mtoto anatakiwa kunyonya angalau kwa kipindi kisichopungua miaka miwili,” amesema Dk. Tulia.
Itakumbukwa kuwa, Anna Makinda, aliyekuwa Spika wa Bunge (2010 -2015), aliwahi kuwambia wabunge wanawake kuwa, wanatakiwa kuwa huru kupata ujauzito na kujifungua katika kipindi cha uongozi wao bila kuhofia kuwa suala hilo linaweza kuwa kikwazo cha utekelezaji wa majukumu yao.
Makinda alieleza hayo katika semina baina yake na wabunge wanawake iliyofanyika katika ukumbi wa Msekwa.
MwanaHALISI online ilimtafuta Mbunge mmoja mwanawake ambaye ni miongoni mwa wenye watoto wachanga, huku akiwa tayari kuzungumza lakini kwa sharti la kutotajwa jina.
Mbali na kupongeza hatua hiyo ya Bunge lakini pia wamesema kuwa chumba ambacho wametengewa na Spika kinahitaji kuboreshwa zaidi na kufanya mazingira yawe rafiki zaidi.
“Chumba hicho kinatakiwa kuwa na maji ya moto kwa ajili ya kuwaogeshea watoto, midori ya kuchezea watoto pamoja na vifaa ambavyo vitakuwa rafiki katika kufulia nguo za watoto. Hapo hakika tutakuwa huru kuweza kukitumia kunyonyesha,” amesema.
Leave a comment