BAADHI ya Wabunge wa Bunge la Jamhuri wamehoji lini serikali itaweka hadharani majina ya waliokopa matreka ili wajulikane? Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(Dodoam).
Alhaji Abdallah Bulembo, Mbunge wa Kuteuliwa (CCM) ameitaka serikali kueleza kama imeishaweka adharani majina ya watu walikopa matrekta kutoka SUMA JKT.
Akiuliza swali la nyongeza bungeni leo tarehe 8 Februari 2019 Alhaji Bulembo amehoji, serikali imechukua hatua gani kwa ajili ya kuweka majina yao adharani kwa wale ambao wanadaiwa matrekta hayo?.
“Kwa kuwa waliokopa materekita hayo ni watumishi wa serikali pamoja na wabunge, je serikali imeweza kufikisha majina ya wabunge kwa spika ili aweze kuwatangaza ndani ya Bunge?” amehoji Alhaji Bulembo.
Ruth Molleli, Mbunge wa Viti Maalum (Chadema) akiuliza swali la nyongeza amesema, kwa kuwa waliokopa matrekta hayo ni watumishi wa serikali pamoja na wabunge, je ni kwanini wadaiwa hao majina yao yasitangazwe katika magazeti ili waweze kujulikana.
Awali katika swali la msingi la Naghenjwa Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki (Chadema) alitaka kujua ni kiasi gani hadi sasa kimerejeshwa kwenye Idara ya Zana za Kilimo.
Mbunge huyo amesema, SUMA JKT Idara ya Zana za Kilimo ilikopesha Sh. 5,355,153,000 kwa idara mbalimbali ndani ya SUMA JKT.
Taarifa ya CAG ya mwaka imeonesha kuwa hadi kufikia 30 Juni 2016 ni kiasi cha Sh. 534,785,000 ambayo ni kiasi chini ya asilimia 10 ndiyo kimerejeshwa.
Akijibu maswali hayo Husein Mwinyi, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa amesema, kuhusu wadaiwa wa SUMA JKT kutangazwa katika magazeti, tayari zoezi hilo lilishafanyika.
Amesema, kutokana na wakopaji wengi kuwa ndani ya taasisi mbalimbali, tayari kila taasisi inayo majina ya wanaodaiwa na wale ambao ni wabunge tayari Ofisi ya Spika inayo majina ya wabunge yao.
Mwinyi amesema kuwa, ni kweli mradi wa zana za kilimo wa SUMA JKT ulikopesha miradi mingine ya SUMA JKT jumla ya Sh. 5,355,153,000 kama ilivyoelezwa katika taarifa ya CAG ya mwaka 2015/16 na kwamba, mpaka kufikia 30 Juni 2016 kiasi cha Sh. 534,785,000 ndicho kilichorejeshwa.
Mwinyi amesema, hadi kufikia 31 Januari 2019 jumla ya Sh. 2,389,082,000 zimerejeshwa katika mradi wa zana za kilimo ambayo ni sawa na asilimia 45 ya fedha zote zilizokopeswa.
Na kwamba, mpaka sasa fedha ambazo bado hazijarejeshwa ni Sh. 2,966,071,000.
Leave a comment