WAANDISHI wa habari nchini Tanzania, wametakiwa kujenga desturi ya kusoma sheria na sera zinazowaongoza ili waweze kuzifahamu kwa lengo la kudai haki zao pindi zitakapokiukwa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 17 Novemba 2022 na Afisa Uchechemuzi wa Chama cha Waandishi wa habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Florence Majani, katika mafunzo ya namna ya kuimarisha usawa wa kijinsia katika masuala ya uongozi, iliyoandaliwa na Shirika la Internews na kufanyika mtandaoni.
Florence amesema, mchakato wa maboresho ya sheria zinazosimamia sekta ya habari ukimalika utasaidia kuimarisha haki za waandishi wa habari kwa kuwa sheria bora zitakuwepo, lakini ili haki hizo ziimarike zaidi inabidi wahusika wazifahamu ili waweze kuzisimamia.
“katika mchakato wa maboresho ya sheria za habari watu wanahamasisha sera ziwepo katika vyombo vya habari, zikiwepo zitasaidia mwandishi kujua kwamba mtu akifanya kosa anaweza kuchukuliwa hatua za kinidhamu,” amesema Florence.
Serikali ya Tanzania iko katika hatua za upitiaji maoni yaliyotolewa na wadau mbalimbali kuhusu marekebisho ya sheria za habari, ambapo hivi karibuni Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, anatarajiwa kukutana nao kwa ajili ya kupitia maoni yao ili muswada wa mabadiliko hayo upelekwe bungeni kwa hatua za mwisho.
Leave a comment