AGNESS Mchau (30), ameibuka mshindi kura za maoni ubunge wa viti maalum Mkoa wa Kilimanjaro kupitia Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) kwa kupata kura 24 kati ya 40. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Mkutano huo wa Mkoa wa Kilimanjaro wa UVCCM umefanyika leo Alhamisi tarehe 30 Julai 2020 ambapo wagombea walikuwa 20 kutoka majimbo tisa ya mkoani humo.
Msimamizi wa uchaguzi huo, Alhaji Kundya ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Moshi (DC), amewataka wagombea wote walioshiriki katika uchaguzi huo na kushindwa kuingia katika kinyang’anyiro hicho kushirikia pamoja ili kukijenga chama na kutokukata tamaa.
”Ukiwa na nia ya kushinda ipo siku utashinda tuu, wenye mafanikio makubwa duniani ni wale waliopita katika vipindi vigumu vya kushindwa bila kukata tamaa, ndugu zangu msikate tamaa,” amesema Kundya
Awali, akijinadi mbele ya wa jumbe wa mkutano huo, Agness amesema, kwa miaka yote ambayo yuko ndani ya chama, amejipima na ameona ana uwezo katika kulitumikia taifa ndani ya chama cha mapinduzi.
Amesema, katika nafasi hiyo ya ubunge, ataanzisha mfuko maalum wa mbunge kwa ajili ya kusaidia jumuiya katika utekelezaji wa kazi mbalimbali pamoja na kuanzisha miradi mbalimbali ili kutoa ajira kwa vijana.
”Endapo nikipata nafasi hii nitajikita katika kuinua uchumi kwa vijana kuanzia ngazi ya kata mpaka mkoa na Taifa ili kuhakikisha tunainua uchumi wa viwanda ili kutoa ajira mbalimbali kwa vijana,” amesema Agness
Leave a comment