VITENDO vya ukatili, mila potofu na mimba za utotoni, vimewaibua na kuwakutanisha wazee wa mila 225 kutoka mikoa tisa nchini na kuunda mtandao utakaosaidia kuleta mabadiliko na kupunguza vitendo hivyo ambavyo vimeonekana kushamili. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo jijini Mwanza, wakati wa mkutano uliowakutanisha wazee kutoka mikoa ya Mwanza, Tabora, Shinyanga, Geita,
Kagera, Mara na Simiyu ili kujadiliana namna bora watakavyoweza kuondoa matukio ya ukatili, ndoa na mimba za utotoni katika jamii.
Chifu Mifungo Charles kutoka Geita, alisema ndoa za utotoni ni tatizo na aliendani na karne ya 21, sambamba na maendeleo ya kidunia hivyo wameungana ili kutoa elimu itakayosaidia kuachana na mila potofu na kufanya yaliyomema .
Mifungo alisema changamoto ambazo watakazozifanyia kazi ni kumaliza suala zima la ndoa za utotoni, wanawake kupewa haki ya kumiliki mirathi pamoja na kuondokana na mila ya utakasaji wanawake kitendo kinachoaminika kuwa ni kuondoa mikosi pindi mke au mme anapofariki jambo ambalo lilikuwa likisababisha magonjwa mbalimbali.
Kineno Maporu kutoka Tabora, alisema vijana wanapaswa kubadilika na kuachana na tamaduni za kizungu, bali waendelee kuishi kwa kufuata mila zao ambazo ni nzuri na zenye tija, japo umaskini ndio chanzo kikubwa cha vijana kubadilika, lakini ushirikiano wao na serikali unahitajika ili kulijenga suala hilo na kuondokana na vitendo vyote vya ukatili.
“Malezi ni jambo la muhimu kuliko yote, hasa kwa mtoto wa kike, wakati mwingine sisi wazazi ndio tunachangia, utakuta mtoto bado mwanafunzi hana kipato chochote, anatumia losheni za bei, mzazi haumuulizi katoa wapi hela, unamuacha hiyo itachangia mtoto kupotea njia na kufuata njia isiyo njema hiyo itachochea mtoto kupenda kuolewa kuliko kusoma,” alisema Maporu.
Kwa upande wake, Lucy Tesha kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa, UN Women kitengo cha kutokomeza ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake hususani watoto wa kike, amebainisha maazimio hayo yaliyowekwa na wazee wa kimila ni moja ya mkakati waliopanga kuunda mtandao wa pamoja kwa mikoa tisa na badala ya kuitwa wazee wa mila waitwe wazee mashuhuri wakiwahamasisha vijana katika mapambano hayo.
Chalya Magaka ni Mganga wa tiba asilia kutoka Kaliua, Tabora, alisema kuwa elimu walioipata watahakikisha wanaenda kuwaelimisha wananchi wenzao kuacha vitendo vya ukatili na kukomesha mimba za utotoni ambazo zinaongezeka nchini kwa kile kinachotajwa ni hali ngumu ya maisha.
Leave a comment