WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema, vitambulisho vipya vya Wamachinga vilivyofanyiwa maboresho vikiwa na picha ya muhusika na baadhi ya kumbukumbu binafsi vitaanza vitaanza kutolewa tarehe 01 Aprili 2021. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Amewataka, Wakuu wa Mikoa (RC) na Wilaya (DC), wahakikishe Wamachinga wanaendelea kufanya shughuli zao bila ya bugudha katika kipindi hiki ambacho muda wa matumizi ya vitambulisho vyao umekwisha.
Majaliwa amesema hayo jana jioni Alhamisi tarehe 28 Januari 2021, wakati alipofunga mkutano na viongozi wa Wamachinga kutoka mikoa yote Tanzania Bara, viongozi wa mabenki na baadhi ya mawaziri na watendaji wa Serikali katika Kituo cha mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam
Alisema vitambulisho hivyo vipya, vilivyofanyiwa maboresho vitakuwa na picha ya muhusika na baadhi ya kumbukumbu binafsi zitakazomtambulisha na kumwezesha kupewa huduma katika maeneo mbalimbali zikiwemo na taasisi za kifedha.
Majaliwa alisema, vitambulisho hivyo vitakuwa na picha ya mhusika, hivyo haitawezekana kutumiwa na mtu mwingine na pia vitadumu kwa miaka miwili hadi mitatu tofauti na vya sasa ambavyo vilikuwa vya mwaka mmoja.
“Serikali kupitia John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeamua kutoa vitambulisho rasmi ambayo vitawatambulisha popote na kupata huduma muhimu kama vile kutambulika na taasisi za fedha na maeneo muhimu,” alisema
Kadhalika, Majaliwa aliwaagiza viongozi wa Wamachinga wahakikishe wanakuwa na takwimu sahihi idadi ya Wamachinga ili iwe rahisi kuwahudumia.
“Tuwe na kanzidata ya Wamachinga itarahisisha mawasiliano ndani ya Shirikisho la Wamachinga na Serikali,” alisema Majaliwa
Waziri Mkuu alisema, Wamachinga wajiunge pamoja kuanzia ngazi ya Vitongoji hadi Taifa ili waweze kuhudumiwa kwa urahisi.
“Mkijiunga pamoja na kutambuliwa ni rahisi kwa taasisi za kifedha kuwafikia na kuwapatia huduma za mikopo itakayowawezesha kukuza mitaji yenu.”
Alisema Serikali imedhamiria kumhudumia na kumtumikia kila mwananchi wakiwemo Wamachinga kwa lengo la kuwawezesha kukuza biashara zao na kujikwamua kiuchumi, hivyo aliwataka wafanye kazi kwa bidii.
Leave a comment