WATANZANIA waishio nchini China, wako njia panda baada ya kukwama kurejea nchini kufuatia mlipuko hatari wa Virusi vya Corona, vilivyopoteza maisha ya watu zaidi ya 1,000. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Baada ya mlipuko huo kuendelea kuwa tishio, Watanzania hao ambao kwa sasa wamefungiwa sehemu moja ili kunusuru usalama wa maisha yao, wameiomba Serikali ya Tanzania kufanya hima kuwarejesha nchini.
Akizungumzia kuhusu suala hilo, Balozi wa Tanzania nchini China, Mbelwa Kairuki amesema Watanzania hao wako katika wakati mgumu kutokana kwamba, mamlaka nchini China zimeshauri wasisafiri kwenda eneo lolote, ili kukwepa kuambukizwa ugonjwa huo.
Balozi Kairuki amesema uamuzi juu ya maombi ya Watanzania hao kurejeshwa nchini haraka, unatakiwa kuangaliwa kwa umakini kutokana na hali halisi iliyokuwepo, ili kukwepa madhara zaidi.
“Uamuzi utakaofanywa lazima uangalie hali halisi, si busara kufanya maamuzi kwa mihemko. Na tujifunze kwa wenzetu hatua walizochukua na matokeo yake. Ili tusijekuwa na majuto makubwa zaidi,” ameshauri Balozi Kairuki.
Balozi Kairuki ameeleza kuwa, hata nchini Japani Watanzania wote walikuwa wazima, lakini walipoanza kuondolewa, wanafunzi watano walipata maambukizi ya ugonjwa huo, ambao pia waliwaambukiza wenzao watano.
Kutokana na changamoto hiyo, Balozi Kairuki amewataka ndugu, jamaa na marafiki wa wanafunzi hao kumuomba Mungu aendelee kuwalinda, huku akiwahimiza kuwapa moyo wahusika, ili wasikate tamaa.
Leave a comment