SIKU 11 zimebaki kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 wa Rais, Wabunge na Madiwani nchini Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Vyama 15 vimesimamisha wagombea urais katika uchaguzi huu wa sita kufanyika tangu kurejea kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini Tanzania mwaka 1992.
Miongoni mwa vyama hivyo 15 ni Chadema ambacho kimemsimamisha Tundu Lissu kuwania urais na kumkabidhi Ilani ya Uchaguzi ya 2020/25 ili kuinadi kwa wananchi.
Ilani hiyo yenye kauli mbiu ya Uhuru, Haki na Maendeleo ya Watu imeainisha vipaumbele 20 itakavyovifanyia kazi kwa miaka mitano endapo kitapata ridhaa ya Watanzania kuongoza Taifa hilo linalounda Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Vipaumbele hivyo ni;
- Kugatua madaraka ya uongozi na utawala kwa lengo la kuusogeza karibu na wananchi
- Kubadili mfumo wa uongozi na utawala ili kuongeza na kuzingatia misingi ya uadilifu, ufanisi, uzalendo na uwajibikaji
- Kwa kushirikiana na sekta binafsi Kujenga uchumi imara wa kidigitali na shirikishi
- Kuongeza mishahara na kuwapandisha madaraja watumishi wa umma
- Kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje
- Kurejesha mchakato wa Katiba Mpya kuanzia ilipoishia Rasimu ya Tume ya Marekebisho ya Katiba ya Jaji Warioba
- Kurejesha uhuru wa vyombo vya habari na uhuru wa kujieleza na kutoa maoni
- Kutoa elimu bora na bure kwa ngazi zote
- Kuanzisha utaratibu wa afya bure kwa akinamama wajawazito, watu wenye ulemavu, watoto na wazee
- Kuwajengea uwezo wanawake kusimamia na kumiliki uchumi
- Kwa kushirikiana na sekta binafsi kuongeza wigo wa ajira na kipato chenye tija kwa vijana
- Kwa kushirikiana na sekta binafsi ili kuhakikisha upatikanaji wa maji safi, salama na ya uhakika kwa wote.
- Kuwezesha Wananchi kumiliki ardhi kwa matumizi endelevu
- Kushirikiana na sekta binafsi kuboresha miundombinu ya barabara, masoko, nishati na viwanda vya kusindika mazao vijijini.
- Kutumia rasilimali ya maji iliyopo kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na mifugo.
- Kushirikiana na sekta binafsi Kuboresha miundombinu ya barabara, reli, usafiri wa anga na majini.
- Kushirikiana na sekta binafsi kuboresha sekta ya utalii na maliasili.
- Kushirikiana na sekta binafsi kuhakikisha uwepo wa Nishati nafuu na ya uhakika.
- Kuboresha sekta ya madini na kuwezesha wachimbaji wadogo wanashiriki na kumiliki uchumi wa madini.
- Kushirikisha sekta binafsi katika kuimarisha sekta ya sanaa, utamaduni na michezo na kuifanya iwe ya kibiashara.
“Ilani hailengi kusheheni ahadi hewa bali dira ya kile serikali ya Chadema itakachotekeleza baada ya kupata ridhaa, kufutilia mbali madhara ya kuwepo kwa dola lililoongozwa na chama dola kilichojiona kuwa juu ya matakwa ya wananchi.”
“Ilani hii imebeba maono na mwelekeo wa kisera wa Serikali ya Chadema kwa lengo la kuwashawishi wapiga kura kuchangua wagombea wa Chadema kwa vile Chadema kinaamini katika “Uhuru, Haki na Maendeleo ya Watu,” inaeleza Ilani hiyo
Leave a comment