SERIKALI ya Tanzania imeshauriwa kuanzisha majukwaa huru yatakayowapa fursa wananchi kuwahoji wagombea wa nafasi za uongozi serikalini, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde,Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Ijumaa tarehe 17 Julai 2020, na Dk. Camilius Kassala, Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Haki za Binadamu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), katika majadiliano ya wadau wa uchaguzi na Taasisi ya Kuzuia na Kuoambana na Rushwa (Takukuru), kuhusu namna ya kudhibiti rushwa katika mchakato wa uchaguzi huo.
Dk. Kassala amesema wananchi wanatakiwa kupewa fursa ya kuhoji mali walizonazo wagombea kabla ya uchaguzi, walizipataje, hasa wale wanaotoa rushwa kwa wananchi kabla ya uchaguzi.
“Kuwe na jukwaa la taifa ambapo wananchi watachangia kujadili suala la rushwa, wapewe fursa ya kuwahoji wagombea udiwani, ubunge na urais, wahoji mali zao walizonazo sasa wamezipataje hasa wanaotoa zawadi nyingi hizo fedha wamepata wapi,” amesema Dk. Kassala.
Dk. Kassala amehoji, “na kwa nini wanatoa muda huu na si wakati wa kawaida ambapo watu walikuwa na shida?. Haya yachukuliwe kwa umakini ili wananchi wajione kuna uhuru hasa uhuru wa kuhoji wagombea.”
Dk. Kassala amesema, michakato ya uchaguzi ndani ya vyama hasa ya kutafuta wagombea, iwekwe wazi kwa wananchi, ili kudhibiti vitendo vya rushwa.

“Sababu vitendo vyote vya rushwa huwa vinafanyika sirini, uwepo mifumo ya uwazi ndani ya vyama hasa upande wa idara za serikali na ngazi zote za taasisi za umma. Kuwe na uwazi ili wananchi waweze kuona,” amesema Dk. Kassala.
Kuhusu mjadala huo ulioshirikisha viongozi wa dini, wanasiasa na taasisi zinazoshughulikia masuala ya siasa na uchaguzi, Dk. Kassala ameipongeza Takukuru kwa kuandaa warsha hiyo kwa kuwa itasaidia kutoa elimu kwa vyama vya siasa juu ya kujiepusha na rushwa.
Soma zaidi..
“Takukuru imetambua kwamba kazi ya kupambana na rushwa ni yetu wote, kwa hiyo kila mmoja ana nafasi. Watu wote kwa pamoja wameona waitwe watu hasa viongozi wa dini, walioitwa kuchangia maadili yanayohusisha uchaguzi mkuu ili kupinga suala la rushwa,” amesema Dk. Kassala.
Naye Alhaji Mussa Salum, Sheikh Mkuu wa Dar es Salaam, amewasihi wanasiasa kujiepusha na vitendo vya rushwa wakati wanaendesha mchakato wa uchaguzi huo.
“Viongozi wanaogombea wamuogope Mungu, Rushwa ni haramu inapofua macho haimpendezi Mungu,” amesema Alhaji Salum.
Aidha, Alhaji Salum amesema mwitikio wa wanasiasa wengi kutia nia za kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi huo, unaashiria kwamba rushwa imepungua, hivyo haki itatendeka katika michakato ya uteuzi.
“Watu wanaona hakuna rushwa ndio maana wimbi kubwa la wenye rika mbalimbali hata viongozi wa dini wanagombea, hii inaonesha Takukuru imesimama vizuri hakuna rushwa,” amesema Alhaji Salum.
Alhaji Salum amesema warsha hiyo imekuja muda muafaka kwa kuwa ni kipindi ambacho rushwa inatamalaki.
“Mkutano huu umekuja kwa wakati mwafaka, Watanzania tusimame imara. Ukichagua mla rushwa umenunuliwa na umeza heshima yako na sisi viongozi wa dini kazi yetu kubwa kuwahofisha watu dhidi ya hofu ya Mungu, wasiogope Takukuru sababu kuna mahali fulani haipo. Wewe unaetaka kutoa rushwa na kupokea muogope Mungu,” amesisitiza Alhaji Salum.
Leave a comment