SERIKALI ya Tanzania, imesisitiza ifikapo Desemba 2022, vijiji vyote vya Tanzania Bara, vitakuwa vimefikishiwa umeme na Wakala wa Nishati Vijijini (REA). Anaripoti Jemima Samwel DMC … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Alhamisi, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Nishati, Steven Byabato, wakati akijibu swali la mbunge wa Bukoba Vijijini, Jasson Rwaikiza.
“Je, ni lini umeme utapelekwa katika Vijiji vya Buzi, Buguruka, Musina, Nsheshe na vingine ambavyo havijafikiwa na umeme katika Jimbo la Bukoba Vijijini,” amehoji Rweikiza
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Byabato amesema, Serikali kupitia REA, inaendelea kupeleka umeme na kufikisha katika vijiji vyote vya Tanzania Bara ifikapo Desemba, 2022.
“Vijiji vinane kati ya vijiji 94 vya Bukoba Vijijini ambavyo ni Buzi, Buguruka, Musira, Nsheshe, Ngarama, Omubweya, Kagarama na Rukoma vinatarajiwa kupatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili,” amesema Byabato
“Mradi huu ulianza kutekelezwa Machi, 2021 na unatarajia kukamilika Desemba, 2022. Gharama ya mradi ni Sh.2.04 bilioni,” amesema
Leave a comment