JUMUIYA Vijana ya Chama cha Wananchi CUF (JUVI-CUF), imemuonya Shaka Hamidu Shaka, Kaimu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) kutokana na kauli alizotoa dhidi ya Maalim Seif Sharif Hamad, Katibu Mkuu wa CUF, anaandika Mwandishi Wetu.
Hivi karibuni Shaka Hamdu alinukuliwa akimtaka Maalim Seif kutoa ushahidi unaothibitisha kuwa alishinda uchaguzi wa Oktoba 2015 kama ambavyo amekuwa akieleza mara kwa mara.
Katika taarifa yao kwa umma, JUVICUF imesema, Shaka Hamdu hana hadhi ya kujibiwa chochote na Maalim Seif na kwamba kama kijana huyo anahitaji ushahidi wa ushindi wa CUF katika uchaguzi wa Oktoba 2015 visiwani Zanznibar basi aiombe serikali ya CCM na makada wake.
“Ushahidi wa ushindi wa CUF Zanzibar umetapakaa kila sehemu. Akamwombe Rais Mstaafu Jakaya Kikwete, akamwombe kada wao Jecha Salim Jecha, akamwombe mwenyekiti wake Dk. John P Magufuli na kama haitoshi akawaombe waangalizi wa uchaguzi wa ndani na nje.” Imesema JUVICUF.
Imemuagiza Shaka kutafuta tamko la JUVICUF Wilaya ya Mjini Unguja la tarehe 02/02/2017, ambapo atakuta majibu ya maswali yake kwani hao ndiyo wenye hadhi sawa na yeye.
“Shaka aache mara moja kasumba za kuwa mwanamume ‘domo zege’ amtakaye mwanamke halafu anakuja na staili za kujifanya anamchukia. Kama kapendezwa na mwenendo wa CUF na anataka uanachama basi alete maombi na kama atakidhi vigezo basi atakubaliwa.”
JUVICUF imemtaka Shaka kuacha kuropoka kuhusu mambo asiyoyafahamu kiundani.
“Anasema maridhiano hayawezekani. Yeye ni nani? Kwani maridhiano kadhaa yaliyopita Zanzibar yalikuwa na kibali chake? Wazanzibar wataipata haki yao iliyoporwa tarehe 28 Octoba, 2015 na kama anabisha amuulize mwenyekiti wake Rais Magufuli au Dk. Ali Mohamed Shein,” imeeleza JUVICUF.
Leave a comment