VIONGOZI watatu wandamizi wa Chama cha Wananchi (CUF), wamekamatwa na jeshi pa polisi, wilayani Kilwa, mkoani Lindi, kwa tuhuma “zisizojulikana.” Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Miongoni mwa waliokamatwa, ni pamoja na Suleman Bungara ‘Bwege,’mbunge wa chama hicho katika jimbo la Kilwa Kusini.
Wengine, ni Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa chama hicho, Mbarala Maharagande, mwenyekiti wa Halmashauri ya Kilwa, Abuu Mjaka na mjumbe wa Kamati Tendaji, Fatuma Karambwe.
Bwege, mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa katika eneo hilo, alikamatwa na wenzake hao, muda mfupi baada ya kumaliza kuhutubia mkutano wa uzinduzi wa kampeni za udiwani kwenye kata ya Kivinje, wilayani Kilwa.
Taarifa zilizothibitishwa na Kaimu naibu katibu mkuu wa chama hicho, Tanzania Bara, Joran Bashange, viongozi licha ya kufikishwa kituo cha polisi, wameshindwa kupewa dhamana.
“Ni kweli kwamba mbunge wetu wa Kilwa Kusini, Sulemani Bwege na viongozi wengine wawili, Maharagande na Mjaka, wamekamatwa na mpaka sasa, bado wanaendelea kushilikiwa na jeshi la polisi,” ameeleza Bashange.
Anasema, “tukio hilo limetokea jana jioni, mara baada ya kumfunga mkutano wa ufunguzi wa kampeni za udiwani kwenye kata ya Kivinje.”
Akiongea kwa uchungu na MwanaHALISI Online, Bashange anasema, “huu ni uonevu mkubwa. Haukubariki kwa vigezo vyovyote vile vya kisheria na kiutu.”
Anasema, aliyeanza kushikiliwa na polisi, ni Maharagande na kwamba Bwege na Mjaka walipopata taarifa hizo, waliamua kwenda kufuatilia, ndipo nao wakakamatwa na kuwekwa ndani.
Uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata ya Kivinje, unafanyika kufuatia aliyekuwa diwani wa kata hiyo, Jafari Arobaini, kuamua kujiuzulu.
Arobaini alitangaza kujiuzulu, mwezi mmoja uliyopita, kwa kile alichokiita, “kumuunga mkono Rais John Magufuli katika juhudi zake za kuiletea Tanzania maendeleo.”
Bwege amekuwa mmoja wa wabunge wanaojenga hoja za nguvu zinazoikosoa serikali ya Rais Magufuli bungeni na kuituhumu kwa mambo kadhaa, ikiwamo “mauwaji, utekaji na utesaji.”
Leave a comment