NAIBU Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega, amesema Vyombo vya Ulinzi na Usalama vinawachunguza baadhi ya viongozi wa Soko la Kimataifa la Samaki Feri, jijini Dar es Salaam, wanaotuhumiwa kwa vitendo vya rushwa. Anaripoti Nasra Bakari, DMC…(endelea).
Ulega ametoa kauli hiyo leo Jumatano tarehe 19 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma, baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Azzan Zungu, kumtaka atoe maelezo juu ya tuhuma za rushwa zinazowakabili viongozi wa soko hilo, hasa katika ukanda wa nane (Zone 8).
Akitoa maelezo ya sakata hilo, Ulega amesema uchunguzi wa tuhuma hizo ukikamilika, watuhumiwa hao watachukuliwa hatua.
“Tumepata taarifa za awali na vyombo vyetu vya dola vinafanyia kazi, wapo viongozi wanaoitwa wa zone namba nane, wanafanya vitendo visivyo vya kiungwana kuwalazimisha wavuvi waweze kutoa rushwa wasajiliwe,” amesema Ulega na kuongeza:
“Hiyo ni kinyume cha sheria, vyombo vyetu vitachukua hatua stahiki na jambo hilo liachwe mara moja. Mamlaka ya Ilala zishughulikie eneo hili na hawa wanaofanya vitendo hivi waache mara moja.”
Awali, Zungu alidai kuwa, baadhi ya wavuvi wameshindwa kusajili vyombo vyao baada ya kudaiwa rushwa ya fedha, na viongozi hao.
“Kuna tatizo Soko la Feri Dar es Salaam, wavuvi wanashindwa kusajili vyombo vyao mpaka wazungumze chini ya meza, hasa zone namba nane, toa maelezo,” alisema Zungu.
Leave a comment