VIONGOZI na wenyeviti wa bodi ya mashirika takribani nane yakiwemo, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), wamekalia kuti kavu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Ni baada ya kutoandaa taarifa za hesabu ili zikaguliwe na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2019/20, ambazo zimewasilishwa bungeni tarehe 8 Aprili 2021.
Leo Ijumaa, tarehe 7 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma, Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema aliagiza taarifa hizo za CAG zipelekwe kwa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) na ile ya Serikali za Mitaa (LAAC), lakini amebaini kuna mashirika hayakukaguliwa, kutokana na kutoandaa taarifa zake.
“Sasa huu ni uzembe wa hali ya juu kwa shirika kukosa hesabu zinazokaguliwa. PAC muyaite haya mashirika, uongozi wa menejimenti na wenyekiti wa bodi, kama hawana sababu za maana, tutatoa ushauri kwa serikali ikiwezekana bodi zivunjwe,” amesema Spika Ndugai.
Mbali na MNH, Tanesco, ameataja baadhi ya mashirika hayo ni Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), Kampuni ya Uwekezaji ya UTT, Shirikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC), Shirika la Posta na Shirika la Reli Tanzania (TRC).
“Muwaite haraka, ni hatari kabisa kwa mashirika kama haya, yanakosa hesabu,” amesema Spika Ndugai na kuongeza;
“Natoa onyo, wakati wa CAG kukagua yawe na taarifa. Tunazilaumu halmashauri kwa kuwa na hati chafu wakati kuna mashirika hayana hesabu.”
Leave a comment