TAASISI ya Vicoba endelevu Temeke imeiomba serikali kuiunga mkono katika jitihada zake za kuanzisha viwanda vidogo, ili kufikia uchumi wa kati kwa wanachama wake na taifa kwa ujumla. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Ombi hilo limetolewa hivi karibuni na wanachama wa taasisi hiyo katika uzinduzi wa jina la Taasisi ya Vicoba Endelevu Temeke, ambalo ni ‘Temeke Pamoja’, uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Mratibu wa Taasisi ya Vicoba endelevu Temeke, Johari Mkonde aliitaka serikali kuwapa eneo kwa ajili ya kuanzisha mashine ya kusaga ikiwa ni miongoni mwa miradi iliyopangwa kutekelezwa na taasisi hiyo.
“Tunaiomba serikali itusaidie kupata eneo, tupo tayari kuchangia gharama kama kutakuwa na uhitaji. Taasisi yetu ina dhamira ya kufikia uchumi wa kati kupitia sekta ya viwanda. Kwa sasa tunahimiza wanachama kujiwekea hisa na kukopa ili kuendeleza miradi mbali mbali ambayo baadhi tumeanza kuitekeleza,” alisema Mkonde.
Mkonde alisema kuwa, tangu kuanzishwa kwa taasisi hiyo, idadi ya vikundi imeongezeka kutoka vikundi 20 kwa mwaka jana hadi kufikia 152 mwaka 2018, na kwamba wana malengo ya kuongeza vikundi na wanachama ili kuongeza idadi ya wanufaika wa Vicoba kupitia ujasiriamali na miradi inayotekelezwa na taasi hiyo.
Naye Rais wa Taasisi ya Vicoba Endelevu nchini, Devotha Likokola aliwataka wanachama wa Temeke Pamoja kujikita katika uanzishaji wa miradi mipya ikiwemo viwanda vidogo ili kufanikisha azma ya taifa ya kufikia uchumi wa kati kupitia sekta ya viwanda vidogo.
Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Felix Lyaniva alipongeza jitihada za taasisi hiyo, na kuwahimiza wanachama wake kutumia huduma za kibenki pamoja na kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha ili wafike mbali.
Leave a comment