CHUO cha Ufundi Stadi (VETA) kimeanzisha kozi itakayozalisha wahitimu watakaosaidia kuchakata na kung’arisha madini ya vito, anaandika Jovina Patrick.
Kozi hiyo inakuja kipindi ambacho hivi karibuni serikali imezuia kusafirisha mchanga wa madini (makinikia) nje ya nchi ili kuuchakata.
Akizungumza kuhusu kozi hiyo, Yona Mwambopa Mkufunzi wa Veta, amesema kozi hiyo kwa mara ya kwanza waliitambulisha miaka mitatu iliyopita ila ikakabiliwa na changamoto za kutokuwa na vitendea kazi vya ufundishaji.
“Kama tungekuwa na vifaa tayari tungekuwa tumeshazalisha wataalam wetu hapa hapa nchini,” amesema Mwambopa.
Mwambopa amesema kwamba mwaka huu wameanzisha tena kozi hii lakini muitikio sio wa kuridhisha.
“Hadi sasa tuna wanafunzi 12 ambao wapo chini ya kadirio la elimu nchini wakati inahitaji wanafunzi wasiopungua 16 na wasiyozidi 20,” amesema.
Amesema sababu ya muitiko kuwa mdogo umetokana na ugeni wa kozi hiyo wengi hawajafahamu faida zake, kwani Watanzania wengi wamekuwa wakisoma kozi baada ya kujua faida wanayopata baada ya kuhitimu.
Mwambopa anasema: “Naamini baada ya mafanikio yatakayopatikana kwa wahitimu hawa itawavutia wengine kujiunga zaidi.”
Leave a comment