UMOJA wa Vijana wa Chama tawala Tanzania (UVCCM), umewaomba radhi Watanzania kwa kauli na matendo waliyotoa katika utawala uliopita wa Hayati John Pombe Magufuli na kusababisha chuki na uhasama. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Radhi hiyo, imeombwa jana Jumapili tarehe 28 Machi 2021, na Mwenyekiti wa UVCCM, Kheri James alipokuwa akizungumza na waandishi jijini Dodoma, ikiwa ni takribani siku mbili kupita, tangu mwenyekiti wao wa zamani, Hayati Magufuli, kuzikwa.
Dk. Magufuli, aliyekuwa Rais wa Tanzania kati ya tarehe 5 Novemba 2015 hadi 17 Machi 2021, alipofikwa na mauti akiwa Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam na mwili wake, kuzikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita, 26 Machi 2021.
Kufuatilia kifo hicho cha Dk. Magufuli (61), aliyekuwa makamu wake, Samia Suluhu Hassan, aliapishwa tarehe 19 Machi 2021, kuwa Rais huku akiwaomba Watanzania kuzika tofauti zao na kusonga mbele kama Taifa moja.
Jana Jumapili, Mwenyekiti huyo wa UVCCM, James alisema, umoja huo una Imani kubwa na Rais Samia kuwa ataliongoza vyema Taifa hilo.
“Tuna uhakika Mama Samia atatuongoza vyema na jukumu letu la msingi ni kuhakikisha dhamira njema ya Rais wetu kuhusu umoja wa Watanzania, haki zao, usawa wao, mwelekeo wao kama Taifa sisi ndio tunakuwa nguzo imara kuhakikisha haya yanatokea.”
“Tusiende kuchochea uadui, kuchochea uhasama, na kama yaliwahi kufanyika sisi wote tuna haki na wajibu wa kuombana radhi na kuanza upya kama Taifa ili kumpa nafasi na fursa Mama yetu kutuongoza, si kwa sababu ya jana yetu tukaharibu kesho yetu aliyojipanga kuikabili vyema,” alisema James.
Katika kusisitiza hilo alisema “yawezekana katika siasa zetu, katika hekaheka zetu za kutofautiana kimtazamo, yako mambo yalitokea huko nyuma yalipelekea umoja wetu na mshikamano wetu ukateteleka.”
“Sisi kama Umoja wa Vijana hatuoni aibu kusema tunaomba radhi kwa hayo tuliyoyatenda na tuko tayari kuyarekebisha ili kutengeneza jukwaa safi kwa Rais wetu kuanza upya akiwa na watu walioshikamana kwa umoja,” alisema.
Miongoni mwa kauli ambazo James aliwahi kuzitoa na kuibua mjadala mkubwa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita mwaka 2015, aliwaonya wapinzani akidai wanakusudia kufanya vurugu kushinikiza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iwatangaze hata kama hawajashinda.
James akihutubia mkutano mkoani Arusha, bila kumtaja jina aliyekuwa anamlenga alisema “…mimi msiponitangaza kitaeleweka, safari hii, safari hiiiiii, wajaze upepo, wewe endelea kuwajaza upepo, wala hatutumii nguvu kubwa ni sindao pyaaaaaaaaaa.”
“Vijana wa Arusha, acheni hii wanawadanganya, achene, acheni, atatangazwa kwa wale walioshinda. Hatuwezi kulazimisha kutangazwa kama utashinda. Anasema, nisipotangazwa nitaingiza watu barabarani, sasa waingize barabarani utaona kutakapochimbika,” alisema James
Hichi kitendo anachozungumzia ni kipi haswa? Kuna haja ya kuchunguzwa na hatua kuchukuliwa