MATUKIO ya utekaji, utesaji na hata kupotezwa yamekuwa yakitikisa nchi kwa sasa huku wananchi wakipiga yowe, yakomeshwe. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Hali hiyo imewaibua wazee wa Chama cha ACT- Wazalendo, wakiitaka serikali kuchukua hatua ikiwa ni pamoja na kukomesha matukio hayo.
Wilson Mushumbusi, mwenyekiti wa wazee wa chama hicho akizungumza na wanahabari leo tarehe 7 Julai 2019, katika ofisi za chama hicho Magomeni jijini Dar es Salaam amesema, kuna kila sababu kwa serikali kuhakikisha matukio hayo yanakoma.
Mzee huyo amekemea hayo huku zikiwa zimepita siku tatu baada ya kupatikana kwa Raphael Ongangi, mfanyabiashara wa Kenya na msaidi wa Zitto Kabwe ambaye aliokotwa Mombasa, Kenya jirani na kwa shangazi yake.
Ongangi alitekwa akiwa na mkewe Dar es Salaam ambapo alikaa kwenye mikono ya watekaji, watesaji kwa zaidi ya siku tano na hatimaye kupatikana Kenya.
Tukio la Ongangi ni sehemu ya matukio ya utekaji yanayotikisa kwa sasa nchini, huku serikali ikieleza kuwa ‘watu wasiojulikana’ bado hajawapatikana.
Mbele ya wanahabari Mzee Mushumbuzi amesema kuwa, vitendo hivyo viovu vinaharibu taswira ya nchini na kuongeza hofu kwa Watanzania.
Amehoji kwamba, inawezekanaje mtu akatekwa mchana na kisha akaa siku nyingi bila serikali kujua, na hata baadaye akasafirishwa nje ya nchi?
“Wakati mwingine watekaji wanakuwa na silaha, halafu wanateka mchana tena hata mbele za watu,?” amehoji Mzee Mshumbusi akisema kuwa, serikali inapaswa kukomesha vitendo hivyo.
Wakati huo huo Mushumbusi ameitaka Serikali iweke usawa kwa vyama vya siasa ili kupatikane haki na kuimarisha Demokrasia.
Amesema ili haki ipatikane kwenye uchaguzi lazima kuundwe Tume huru isiyopendelea au kuwa na maslahi kwenye chama chochote cha siasa.
Leave a comment