RAIS John Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amehoji, mtu anawezaje kupata mtoto bila kusogeleana? Anaripoti Hamisi Mguta, Dodoma … (endelea).
Akizungumza baada ya kurejesha fomu ya kugomba kuteuliwa na chama chake –CCM – leo tarehe 30 Juni 2020, kwenye makao makuu ya chama hicho jijini Dodoma amesema, watu wameendelea kusogeleana na maisha yanakwenda.
Alikuwa akizungumzia utaratibu ambapo sasa unasisitizwa duniani wa kukaa umbali wa zaidi ya mita moja, ili kuepuka kueneza virusi vinavyosababisha homa ya mapafu vya corona (COVID-19).
“Unaambiwa usimsogelee mtu mpaka mita moja, mke wako utaacha kumsogelea? au mume wako, utapataje mtoto bila kusogeleana? Nasema uongo?” Rais Magufuli alihoji ambapo alijibiwa “kweliiii!”
Amesema, Mungu ameendelea kusimamia taifa hili na hivyo kusaidia kupungua kwa maambukizi huku akisisitiza Watanzania kuendelea kumuomba Mungu.
“… na ndio maana sisi tukasema, tunaendelea kusogeleana kwa sababu Mungu wetu anatupenda na siku zote anasimama mbele…, leo tupo hapa hatujavaa chochote,” amesema.
Rais Magufuli amerejesha fomu hizo leo ambapo amepokelewa na kupokelewa na Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa chama hicho. Hafla hiyo fupi imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CCM, serikali na wanachama wa chama hicho.
Zaidi ya wanachama milioni moja (1,000,000) wa CCM kutoka mikoa 30, wamejitokeza kumdhamini Rais Magufuli katika safari yake ya kusaka awamu ya pili ya kuliongoza taifa.
Rais Magufuli aliyechukua fomu ya kugombea urais wa Tanzania tarehe 17 Juni 2020, anarudisha fomu hiyo leo katika Ofisi za Makao Makuu ya CCM jijini Dodoma.
Mkoa wa Tanga wamejitokeza wanachama 62,869, Tabora (29,486), Songwe (11,744), Simiyu (3,693), singida (13,452), Dodoma (44,415), Pwani (20,603), Rukwa (5,600), Ruvuma (56,350), Shinyanga (12,000), Arusha (22,706), Dar es Salaam (71,491).
Mtwara (7,569), Mwanza (17,810), Geita (89,595) na Iringa (12,542), Kagera (27,245), Katavi (5071), Morogoro (117,450), Kaskazini Pemba (2,575), Kaskazini Unguja (1,141), Kigoma (30,220), Kilimanjaro (23,434).
Mkoa wa Mjini (2,394), Kusini Pemba (350), Lindi (9,515), Mkoa wa Magharibi (1,005), Manyara (19,972), Mara (87,550) na Mbeya 19,972.
Leave a comment