KWA mara ya kwanza Urusi imetangaza vifo vya wanajeshi wake 498 na wengine 1,597 kujeruhiwa tangu kuanza kwa vita kati yake na Ukraine. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea)
Idadi hiyo inatofautiana kwa mbali na ile iliyotolewa na Jeshi la Ukraine ambapo lilidai wanajeshi 5, 840 wa Urusi wameuawa katika vita hiyo hadi sasa.
Pia Idara ya Usalama ya Uingereza katika taarifa yake ya kile kinachoendelea nchini Ukraine, imeonesha mashaka dhidi ya idadi iliyotolewa na Urusi.
Uingereza imedai kwamba Wizara ya Ulinzi ya Urusi imelazimishwa kutaja idadi hiyo ndogo na kwamba kuna uwezekano madhara ni makubwa zaidi kwa jeshi hilo.
MILIPUKO ZAIDI KYIV
Wakati hayo yakijiri, milipuko zaidi imeripotiwa katikati ya mji mkuu wa Ukraine, Kyiv na video katika mitandao ya kijamii zinaonesha milipuko mikubwa ya rangi ya machungwa angani.
Takribani milipuko minne imeripotiwa usiku wa kuamkia leo Alhamisi Machi 3, 2022.
Katika hatua nyingine jeshi la Ukraine limesema bado jiji la Mariupol lipo mikononi mwao na kwamba jeshi la Urusi halijafanikiwa kulitwaa.
Mji huo umeshuhudia mashambulizi mengi kutoka Urusi na unaonekana kuwa muhimu kwao kwani utawasaidia kuiunganisha na Ukreini upande wa kusini na mashariki.
Leave a comment