Taarifa za hivi karibuni kabisa zinasema, Membe ambaye alishika nafasi hiyo ya uwaziri kwa miaka minane ya utawala wa Jakaya Mrisho Kikwete, ameapa kujitosa katika kinyang’anyiro cha urais kumpinga rais wa sasa, John Pombe Magufuli.
“Kuhusu suala la urais, hilo halina mjadala. Tuombe Mungu niwe mzima. Nitajitosa na nitashinda,” amenukuliwa mwanasiasa huyo akieleza baadhi ya wafuasi wake wa karibu ndani ya chama hicho tawala.
Amesema, “katika hili, siwezi kurudi nyuma na hayupo atakayeweza kunishawishi kurudi nyuma. Nitagombea. Nitajitosa katika kinyang’anyiro hicho kwa kuwa nina sababu ya kufanya hivyo.”
Mbali na viongozi hao, taarifa zinasema, kuna kundi jingine kubwa la wabunge wa chama kilichoko madarakani na hata kutoka upinzani, wanaomuunga mkono Membe.
Kupatikana kwa taarifa kuwa Membe amepanga kujitosa katika mbio za urais 2020, kutaweza kumaliza minong’ono ya muda mrefu kuwa kiongozi huyo amekuwa akiendesha mikakati yake kimya kimya ya kumkabili Magufuli ifikapo 2020.
CCM wamekuwa na utaratibu wa kumpitisha bila kupingwa rais aliyemaliza muhula wake wa kwanza wa miaka mitano, kuchukua tiketi ya kugombea urais tena kwa miaka mitano ya mwisho kikatiba bila kupingwa.
Ndugu yangu Kibajaji Lusinde safiri salama na urejee salama ili utekeleze maagizo uliyopewa ya kunishambulia. Niguse ninuke!
— Bernard K. Membe (@BenMembe) July 20, 2019
Rais aliye madarakani kwa sasa, John Magufuli atamaliza muhula wake wa kwanza 2020 na atarajiwa kuomba tena ridhaa ya chama chake kuwania urais kwa miaka mitano mingine.
Membe alikuwa mmoja wa wagombea urais ndani ya CCM mwaka 2015. Jina lake halikuweza kupenya kwenye vikao vya uteuzi. Tangu wakati huo, amekuwa kimya na kutojishughulisha na masuala ya kisiasa.
Hata hivyo, hivi majuzi baada ya kutajwatajwa na baadhi ya magazeti yanayomuunga mkono Rais Magufuli, Membe ameibuka kujibu kila hoja, ikiwamo inayomhusisha na waraka wa makatibu wakuu wastaafu, Abdulrahaman Kinana na Yusuf Makamba, jambo ambalo limempa heshima kubwa mbele ya jamii.
“Baadhi yetu, tunamuona mheshimiwa Membe kama Mussa aliyekuja kuwakomboa watu wa Misri. Waliamua kumhusisha na kina Kinana na Makamba wakidhani kuwa atanyamaza. Ndio kwanza wametia mafuta kwenye petroli,” ameeleza mbunge mmoja wa CCM ambaye hakupenda kutajwa jina lake.
Tayari baadhi ya wafuasi wake wameanza kuendesha kwa nguvu kampeni iliyopewa jina la “Kazi na Bata,” ili kuvutia wapigakura.
Leave a comment