WANACHAMA wanne kati ya 11 wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ‘wameingia’ mitini katika kinyang’anyiro cha kuomba kuteuliwa na chama hicho kugombea urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Wanachama hao walikuwa miongoni mwa 11 waliotia nia kuwania urais ndani ya chama hicho lakini hawakujitokeza kuchukua fomu pindi shughuli ya uchukuaji na urejeshaji ilipoanza tarehe 4 hadi 19 Julai 2020.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Chama cha Chadema, Rebby Munisi amesema hadi kufikia leo Jumapili saa 10:00 jioni watia nia saba tu wa urais ndani wamechukua na kurejesha fomu.
Amesema, watia nia waliochukua na kurejesha fomu ni Wakili Simba Neo, Aliyekuwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, Mchungaji Leonard Manyama, Dk.Maryrose Majinge, Wakili Gaspar Mwanalyela, Lazaro Nyalandu na makamu mwenyekiti wa chama hicho Bara, Tundu Lissu.
“Tunaendelea kupitia na kujiridhisha kuwa fomu zao walizorudisha zipo sawa na tarehe 22 tutakuwa na mchakato wa kuanza kuchuja wagombea na mkutano Mkuu utafanyika tarehe 29 Julai 2020 kwa ajili ya kuamua nani atapeperusha bendera ya chama kwa upande wa urais,” amesema Munisi.
Miongoni mwa watia nia ambao hawakuchukua fomu za urais ni pamoja na Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Nalo Opiyo na Msafiri Shabani.
Leave a comment