WAKILI Simba Neo, aliyejitosa katika kinyang’anyiro cha Urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amemwaga sera zake. Anaripoti Hamis Mguta,Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na wanahabari leo Ijumaa tarehe 19 Juni 2020 jijini Dar es Salaam, kuhusu sababu za yeye kutaka kugombea urais, Wakili Simba amesema, anataka kurejesha heshima ya Tanzania katika jumuiya za kimataifa.
Amesema atafanya hayo endapo atapata ridhaa ya chama chake kugombea nafasi hiyo, kisha kupata baraka za Watanzania, kuwa Rais wa Tanzania.
Simba amesema, zaidi kilichomsukuma kuwa na nia hiyo, ni Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli, heshima ya Tanzania katika jumuiya hizo, iliyojengwa na Baba wa Taifa, Hayati Julius Nyerere, imeshuka, kutokana na kukithiri kwa vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu.
Amesema, katika uongozi wa serikali zilizopita, nchi ya Tanzania haikuwahi kusemwa vibaya kutokana na ukiukwaji wa misingi ya haki za binadamu, lakini kwa sasa inatia aibu, kutokana na baadhi ya viongozi wake kuwekewa vizuizi vya kusafiri nje ya nchi.
“Wakati wa Mwalimu Nyerere tulikuwa tunasifika, lakini heshima yetu kimataifa imeshuka, hadi kuna mtu amekatazwa kuingia Marekani kuhusiana na ukiukwaji wa haki za binadamu, lakini bado ni mkuu wa mkoa, ingekuwa tunathamini haki za binadamu asingebaki katika madaraka,” amesema Simba.
“Sijawahi kuona tangu marais waingie kuna mtu amewekea ‘persona non grata’ kwa sababu ameenda kinyume na haki za binadamu ni aibu, sitavumulia uvunjwaji wa haki za binadamu hata awe na cheo kaisi gani.”
Sambamba na hilo, Wakili Simba amesema, endapo atafanikiwa kuwa Rais wa Tanzania, atapambana na vitendo vya rushwa pamoja na kuimarisha demokrasia na utawala wa sheria.
“Maendeleo au usalama ili vidumu vinahitaji kuwepo demokrasia na haki za binadamu, huwezi kufanya kimoja ukasahau demokrasia ukategemea kwamba nchi itakuwa salama haiwezekani, “ amesema Wakili Simba na kuongeza:
“Kwa sasa Tanzaniani kama binadamu anaetembea kwa mguu mmoja, tumezama katikamaendeleo tumeacha nyuma demokrasia,” amesema.
Leave a comment