KAZI ya upembuzi wa barabara ya Barabara ya Kinyata kutoka Nyamagana – Usagara, jijini Mwanza yenye urefu wa kilomita 22, inafanyika ili kuitanua na kuwa ya njia nne. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
“Kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii unaendelea, ambapo umezingatia kupanua barabara hii kuwa na njia nne kuanzia Mwanza hadi Usagara,” ameeleza Dk. Leonard Chamuliho, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi.
Dk. Chamuliho ametoa maelezo hayo leo Jumatatu tarehe 12 Aprili 2021, baada ya Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana (CCM) katika kipindi cha maswali na majibu bungeni jijini Dodoma, kutaka kujua hatua iliyofikiwa na serikali katika maandalizi ya ujenzi huo.
Mabula ameuliza “je, ni lini serikai itaanza ujenzi wa barabara ya Kinyata kwa njia nne kutoka Mwanza Jiji kuelekea Usagara?”
Dk. Chamuliho amesema, barabara hiyo ni sehemu ya barabara Kuu ya Mwanza – Shinyanga (mpakani) yenye urefu wa kilometa 104.
“Barabara hii ni muhimu katika kukuza uchumi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa na ni kiunganishi kati ya mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Mara na Geita na nchi jirani. Serikali tayari imeanza mipango ya kuanza ujenzi wa barabara ya Mwanza hadi Usagara kwa njia nne.
“Kazi ya Upembuzi Yakinifu na Usanifu wa Kina wa barabara hii unaendelea ambapo umezingatia kupanua barabara hii kuwa na njia nne kuanzia Mwanza hadi Usagara (km 22).
Dk. Chamuliho amesema, kazi hiyo inafanywa na Mhandisi Mshauri M/s NIMETA Consult (T) Ltd ya Tanzania kwa gharama ya Sh. 980.84 milioni.
Na kwamba, usanifu wa kina unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, 2021 na baada ya kukamilika, barabara hiyo itaingizwa kwenye mpango wa ujenzi.
Leave a comment