BENKI ya NMB kupitia bidhaa yake ya ‘Makazi Loan’ kwa kipindi cha miaka mitatu imetoa zaidi ya Sh.35 bilioni kuwezesha Watanzania kupata mikopo ikiwa ni utekelezaji wa dhamira ya benki hiyo katika kuendeleza ujenzi wa nyumba nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamesemwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Benki ya NMB, Benedicto Baragomwa wakati wa semina iliyowakutanisha wadau mbalimbali wa mnyororo wa thamani ya sekta ya ujenzi iliyoandaliwa na benki hiyo jijini Dar es Salaam.
Alisema bidhaa hiyo ya ‘Makazi Loan’ imeundwa ili kuongeza fursa za umiliki wa nyumba huku akisitiza inaunga mkono jitihada za Serikali za kuhakikisha makazi bora kwa Watanzania wote.
Baragomwa alisema bidhaa hiyo ya benki hiyo inalenga watu kuanzia ngazi ya chini na inatoa fursa mbalimbali kwa wateja katika kununua, kujenga, kumaliza au kupata fedha kwa thamani ya nyumba.
“Lengo letu ni kutoa suluhisho za bei nafuu. Tunaelewa soko la sasa la nyumba lina ushindani wa hali ya juu na hivyo kuifanya iwe vigumu sana kwa wanunuzi wa nyumba watarajiwa hasa wale wenye kipato vya chini,” alisema
Alisema bidhaa yetu ya ‘Makazi Loan’ imeundwa ili kupunguza mzigo kwa mkopaji, kutoa usawa zaidi katika mchakato wa kukopesha nyumba na kuifanya ndoto ya kila Mtanzania kumiliki nyumba itimie.
Baragomwa alisema benki ina mizania yenye nguvu hali ambao inadhiririshwa na utendaji wake mzuri wa kifedha wa nusu mwaka ambapo benki iliripoti faida ya Sh 208 bilioni wiki hii.
“Mikopo yetu ya nyumba inalenga watu wote kuanzia ngazi ya chini. Tuko tayari kutoa mikopo ya nyumba kuanzia milioni 10 hadi milioni 700 na tutaendelea kufanya kazi kwa karibu na wadau wote wa sektta ya ujenzi ili kuhakikisha kuwa Watanzania wote wanamiliki nyumba,” alisema.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Heri James akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makala alisema uzinduzi wa bidhaa ya mkopo wa benki hiyo ya makazi ni muhimu na umekuja wakati muafaka hasa katika kipindi hiki ambacho mkoa huo upo mbioni kuanza yaani ‘Master Plan’.
“Utafiti wa Benki ya Dunia ulionyesha Tanzania ina upungufu wa nyumba milioni tatu na kila mwaka kuna ongezeko la mahitaji ya nyumba laki mbili. Kwa sasa, sekta ya ujenzi inakua kwa kasi lakini ukuaji wa aina hii utakuwa na matunda iwapo benki zitatoa mikopo ya riba nafuu,” alisema
Alibainisha kuna kesi nyingi za ardhi jijini Dar es Salaam ambazo zimesababishwa na wamiliki wa ardhi kushindwa kuendeleza ardhi zao kwa sababu ya ukosefu wa fedha na kuongeza mikopo ya Makazi ya NMB sasa itasaidia kutoa suluhisho ya changamoto hiyo.
“Hii sasa ni fursa adimu kwa watu ambao mashamba yao yamekaa muda mrefu bila kufanyiwa maendeleo yoyote. Jambo zuri ni kwamba mtu anaweza kujadiliana na benki vigezo na masharti. Tuchangamkie fursa hii na tuipatie ardhi yetu thamani,” alisema
Naye Meneja wa mikopo ya nyumba wa Benki ya NMB, Miranda Lutege wakati wa hafla hiyo alisema benki yake itafanya kampeni maalum ya ‘nyumba kwa nyumba’ nchi nzima ili kuhamasisha umma kuhusu suala hilo la makazi bora na fursa zilizopo katika sekta ya ujenzi.
Alibainisha ili kupata mkopo wa nyumba, mtu anatakiwa kuwasilisha makadirio (BoQ), hatimiliki ya ardhi na kibali cha ujenzi.
“Mikopo hii ya nyumba ipo wazi kwa Watanzania wote ndani na nje ya Tanzania (diaspora) na muda wa marejesho ya mkopo unaweza kwenda hadi miaka 15 kulingana na masharti yaliyokubaliwa na pande zote mbili,” alisema.
Leave a comment