SERIKALI ya Tanzania, imejikita katika kukamilisha ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Sumbawanga kilichopo mkoani Rukwa. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Jumatano, tarehe 12 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara, wakati akijibu swali la Mbunge wa Kalambo, Josephat Kandege.
“Je, mpango wa serikali wa ujenzi wa uwanja wa ndege eneo la Kisumba wilayani Kalambo, umefikia hatua gani kwa sasa?” ameuliza Kandege.
Waitara amesema, miongoni mwa viwanja vinne vilivyofanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na kupata ufadhili kutoka Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB), ni kiwanja cha ndege cha Sumbawanga, Rukwa.

Amesema, aidha serikali imekamilisha taratibu za kupata mkandarasi na kupewa idhini kutoka EIB, kinachosubiriwa ni kupata fedha baada ya taratibu za kimkataba kukamilika.
“Baada ya kukamilisha ujenzi wa viwanja vya ndege vya mikoa vilivyosalia ikiwemo Sumbawanga, serikali itaendelea na ujenzi wa viwanja vingine vidogo kwa hadhi ya airstrip ikiwa ni pamoja na kiwanja cha ndege cha Kalambo.
“Napenda kuwashauri wananchi wa Kalambo kutumia kiwanja cha ndege cha Sumbawanga mara ujenzi wake utakapokamilika,” amesema Waitara.
Leave a comment