IMEELEZWA kuwa vitendo vya uvunjifu wa maadili kwa wauguzi na wakunga pamoja na ‘vishoka’ ambao wamekuwa wakijiingiza katika taaluma hiyo bado ni kikwazo katika sekta ya afya nchini. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma… (endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 18 Machi 2023 na Msajili wa Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania (TNMC), Agnes Mtawa jijini Dodoma wakati wa mahafali ya saba na utoaji wa vyeti vya usajili na leseni kwa wauguzi na wakunga zaidi ya 1,000 waliofanya vizuri kwenye mitihani iliyoandaliwa na TNMC.
“Pamoja na mafaniko tuliyoyapata lakini bado zipo changamoto mbalimbali ikiwemo vitendo vya uvunjifu wa maadili kwa wauguzi na wakunga, lakini pia lipo tatizo la watu ambao siyo wanataaluma kuingilia taaluma yetu”amesema.
Ameeleza kuwa wauguzi na wakunga wanapaswa kuzingatia maadili ili kuondoa malalamiko ambayo yamekuwa yakijitokeza katika maeneo mbalimbali ili kupunguza vifo vya mama na mtoto ambavyo vomekuwa vikijitokeza.
Amesema serikali itaendelea kuchukua hatua kwa muuguzi au mkunga yeyote ambaye atabainika kuwa amekiuka maadili kwa kumfuta kwenye usajili.
Aidha, ameeleza kuwa tangu mwaka 2016 wauguzi na wakunga 50 walibainika kuvunja maadili ya utumishi wa umma ambapo kati yao wanne walifutiwa usajili wao na kupokonywa leseni na wengine kupewa karipio kali.
Pamoja na mambo mengine ameeleza kuwa bado kuna kero ya wauuguzi na wakunga vishoka ambao siyo wanataaluma wa afya.
“Bado tuna changamoto kubwa kwani wananchi ambao wanajifanya wanataaluma hii na kutoa huduma bila ya kuwa na vigezo hili ni kosa la jinai, ambao tumekuwa tukiwabaini tumewachuklia hatua za kuwapeleka mahakamani na wengine tayari wameshafungwa vifungo mbalimbali”amesisitiza Mtawa.
Amesema kwamba ili kukabilina na kero hiyo Baraza limeandaa mfumo ambao limewapatia waajiri ili waweze kuhakiki usajili ya wauguzi na wakunga.
“Mfumo huu unaouwezo wa kubaini muuguzi au mkunga aliyesajiliwa na asiyesajiliwa hivyo nitoe wito kwa waajiri kufanya uhakiki kupitia mfumo huu mara kwa mara ili kukabili changamoto ya watu wasio wanataaluma kujipenyeza”amesema.
“Hadi sasa wauguzi na wakunga waliosajiliwa nchini ni 55,000 lakini wenye leseni zilizo hai ni 42,000 ambao wanatoa huduma katika vituo mbalimbali vya serikali na binafsi.
Naye Muuguzi mkuu wa serikali, Ziada Sellah amewataka wauuguzi na wakunga kuacha tabia ya kuchangia maeneo ya kwenda kufanya kazi.
Amesema wanapaswa kufahamu kuwa watu wenye mahitaji wapo nchi nzima hivyo hawanabudi kuchagua maeneo ya mijini kwenda kufanya kazi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza hilo, Prof. Lilian Mselle amesema wataendelea kuchukua hatua kwa mtumishi yeyote ambaye ataoneka kuitia doa taaluma hiyo kwa kufanya vitendo vya uvunjifu wa maadili.
Leave a comment