Thursday , 28 March 2024
Home Habari Mchanganyiko Ukatili na unyanyasaji wa kijinsia unavyoathiri watoto Iringa
Habari Mchanganyiko

Ukatili na unyanyasaji wa kijinsia unavyoathiri watoto Iringa

Mkuu wa wilaya ya Iringa Mjini, Richard Kasesela akimfundisha mmoja wa wanafunzi wa shule ya msingi Kihorogota
Spread the love

LICHA ya juhudi za serikali na watetezi wa haki za watoto kuendeleza harakati za kulinda hadhi na afya za watoto nchini Tanzania, matukio ya unyanysaji na ukiukwaji wa haki za watoto bado ni tatitizo sugu mkoani Iringa. Anaripoti Faki Sosi.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi maalumu wa habari za watoto nchini umegundua kukithiri kwa vitendo vya unyanyasaji dhidi ya watoto, hasa ubakaji na ulawiti mkoani humo, hasa wilaya ya Iringa Mjini ambayo pia ni Manispaa ya Mji wa Iringa.

Mkuu wa Wilaya ya Iringa Richard Kasesela amesema alipozungumzia moja kati ya matukio ya ubakaji kuwa tatizo hilo linachangiwa na vitendo vya watendaji wasio waaminifu kufumbia macho uovu huo unapotokea katika maeneo yao ya kazi.

Kasesela amesema pia kuna askari wanaoshindwa kutekeleza majukumu yao na hivyo kuachia matukio hayo kupita bila kuchukua hatua za kuwakamata wahalifu kasha kuwafikisha katika vyombo vya sheria ili kuchukuliwa hatua za kisheria.

Mwenyekiti wa taasisi inayoshughulika masuala ya vijana na watoto iringa mjini ya Action Ministry Bw. Samwuel Kadege ameeleza kuwa wazazi na wanajamii wamekuwa chanzo cha kuficha matukio ya ulawiti na ubakaji kutokana na kuyamaliza masuala hayo kifamilia.

Kwa mujibu wa Bw. Kadege, inapotokea tatizo la ubakaji na ukatili dhidi ya watoto, familia husika hukaa kimya bila kushughulikia tatizo hilo kwa taratibu za kisheria na hivyo kumalizwa kwa njia za kimila na kifamilia.

Bw. Kadege amesema kwamba wazazi, walezi na jamii ndani ya mkoa wa Iringa ndio chanzo kikubwa cha tatizo la ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto wa jinsia zote.

Uchunguzi wa vyombo vya habari mkoani Iringa umeonesha kuwa vyanzo vikuu vya kuendelea kwa matukio ya ukatiki kwa watoto huchangiwa na tabia ya kufungua milango ya suluhu nje ya vyombo vya kisheria na ukimya uliokithiri katika familia nyingi.

Umasikini na ukosefu wa elimu pia ni vikwazo vinavyosababisha kuongezeka kwa ukatili dhidi ya watoto mkoani humo, hali inayosababisha matukio ya ulawiti na ubakaji kumalizwa kwenye meza ya mazungumzo ndani ya familia ua kati familia na familia.

Mazungumzo ndani ya familia pamoja na ukimya ni hali inayosababisha kupoteza ushahidi na pia kupoteza haki za kisheria dhidi ya watoto wanaofanyiwa vitendo hivyo viovu, kwa mujibu wa Mchambuzi wa masuala ya Kijamii Martin Kilowela.

“Tatizo la ukatili wa kijinsia mkoani Iringa yanatakiwa yawepe kipaumbele kuyamaliza. Kama waathirika watatoa taarifa katika vyombo vya dola, tunaamini kwamba tatizo hilo litashughulikiwa kwa taratibu za kisheria na haki kutendeka”, amesema Bw. Kilowela.

Kwa mujibu wa Bw. Kilowela, ubakaji na ulawiti ni kosa la jinai ambalo maamuzi yake hutolewa na mahakama chini ya sheria ya Makosa ya Kijinsia iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwa 1998 ambayo kwa sasa inatumika nchini kote.

“Tabia ya wazazi kufumbia macho ukatili huu au kukaa kimya bila kuchukua hatua za kisheria ni kosa kubwa linalochochea kasi ya kuongeza ukatili wa kijinsi mkoani Iringa”, amesema Bw. Kilowela.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Iringa David Ngunyale amesema kuwa kesi za ukatili dhidi ya watoto hukwamishwa na wanafamilia kushindwa au kukataa kufungua jalada la mashtaka mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake.

Badala ya kutoa taarifa vituo vya Polisi ili watuhumiwa wakamatwe na kufunguliwa shauri la jinai mahakamani, familia iliyoathirika na uovu huo hukaa chini na kufanya upatanishi kati yake na mtuhumiwa.

Hakimu Ngunyale amesema kitendo cha familia au wazazi wa mototo aliyedhalilishwa kwa njia ya ngono kumaliza matatizo hayo kifamilia ni kosa linalochochea ongezeko la vitendo vya ubakaji na ulawiti mkoani Iringa.

“Tabia iliyozoeleka ya wazazi kumaliza matatizo ya ubakaji, ulawiti na unyanyasaji wa kijinsia mitaani ni kibaya kwa kuwa muathirika hukosa haki yake na pia vitendo hivyo kuendelea kufanyika mkoani hapa bila kikomo”, amenukuliwa Hakimu Ngunyale.

Hakimu Ngunyale amesema kuwa ushahidi kupindishwa au mashahidi kutofika mahakamani kabisa, ni jambo linalosababisha kesi za jinai kuhusu udhalilishaji kushindikana na hivyo sheria kushindwa kuchukua kukunjua makucha yake.

Amesema kuwa mara nyingi kesi hizo hutokea ndani ya familia ambapo inapelekea wanafamilia kumalizana wao kwa wao na wakifika Mahakamani wanapindisha ushahidi.

Akitoa mfano mm oja wa kesi iliyowahi kufika Mahakamani hapo, Bw. Ngunyale alisema kuwa mtuhumuwa alikuwa baba wa kambo aliyembaka mtoto wa mke wake, baadaye kesi hiyo ilishindwa kuendelea baada ya yule mtoto kubadilisha ushahidi Mahakamani kuwa hajabakwa na yule baba na kumtaja mtu mwengine ambaye hayupo.

“Tatizo hilo linaanza kwenye mikono ya wazazi na wanajamii ambapo ametoa wito kwa jamii kutoa ushidi na ushirikiano kwa ili kutokomeza ukatili kwa watoto”, Hakimu Ngunyale ameongeza kusema.

Inakadiriwa kuwa takribani vitendo kati ya 120 na 145 vya udhalilishaji wa kijinsia kwa njia ya ubakaji na ulawiti hutokea Wilayani i Iringa kila mwaka ambapo watuhumiwa kati ya 100 hadi 108 wanajulikana kuhusika na unyama huo.

Kutokana na kushamiri kwa vitendo hivyo, Serikali wilayani Iringa imesambaza waraka unawataka wazazi na walezi kutowatuma watoto eneo lolote kuanzia kuanzia saa 12.00 jioni miaka ya hivi karibuni.

Kutokana na kukithiri kwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto nchini, serikali kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) imezindua Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya wanawake na Watoto kati ya mwaka 2017 hadi 2022 unaolenga kokomesha ukatili kwa wanawake na watoto.

Mpango Kazi huo shirikishi umelenga hasa kufuatilia masuala ya misaada ya sharia kwa waathirika wa vitendo vya ukatili wa kijinsia, utoaji huduma kwa wahanga na uratibu wa matukio ya ukatili na udhalilishaji kwa makundi husika.

Waziri wa Afya, Maendeleo Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema haridhishwi na namna ambavyo mahakama zimekuwa zikishughulikia kesi za vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto kutokana na kesi hizo kuchukua muda mrefu kumalizika wakati takwimu za matukio yanayotokana na vitendo hivyo yanazidi kuongezeka.

Akielezea juu ya takwimu kutoka Jeshi la Polisi, Waziri Mwalimu amesema vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto vilikuwa 22,876 mwaka 2015 ambapo ubakaji pekee kulikuwa na waathirika 3,444 waliotoa taarifa vituo vya polisi.

Akitoa taarifa ya vitendo vya ukatili dhidi ya watoto mwishoni mwa mwaka jana (2017), Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Kamishna wa Polisi Bw. Robert Boaz amesema kwamba jumla ya makosa ya ubakaji 7,460 yameletwa katika vituo kadhaa vya polisi nchini kote.

Kamishna Boaz amesema kwamba makosa hayo ni pamoja na ubakaji na ulawiti ambapo makosa ya ulawiti yaliyopelekwa katika vituo vya polisi kati ya Januari na Novemba mwaka huo ni 25 ambayo ni ongezeko la waathirika 9 kutoka 16 waliofunguliwa majalada vituo vya polisi mwaka juzi.

Kamishna Boaz amesema kuwa makosa ya ubakaji mwaka jana ni ongezeko la vitendo 478 kutoka 6,985 mwaka uluiotangulia.

“Vitendo vya ubakaji na ulawiti vimeshamiri kutokana na mmomonyoko wa maadili na tamaa mbay za mwili, pamoja na imani potofu za ushirikina ndani ya jamii yetu hapa Tanzania. Napenda kuwaasa wananchi wote wawe na maadili mema na pia waachane na imani za kishirikina,” ameshauri Kamishna Boazi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari Mchanganyiko

Wafanyabiashara, wawekezaji China waridhia kuwekeza bil. 800 katika sekta 5 nchini

Spread the loveUJUMBE wa wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa kutoka Jimbo la Changzhou...

Habari Mchanganyiko

Bil. 4.42 kumaliza uhaba maji kata 2 Musoma Vijijini

Spread the loveWANANCHI wa kata za Busambara na Kiriba, Jimbo la Musoma...

BiasharaHabari Mchanganyiko

Soko nepi za watoto lashuka, watu wazima lapaa

Spread the loveKiwanda cha kutengeneza nepi cha Japan kimetangaza kuwa kitaacha kutengeneza...

Habari Mchanganyiko

NMB yafuturisha Dar, Majaliwa azitaka Serikali za Mitaa, Taasisi zijifunze kwao

Spread the loveBENKI ya NMB imewafuturisha wateja wake walio kwenye Mfungo wa...

error: Content is protected !!